Habari za Kitaifa

Wanafunzi wamaliza wiki nzima bila kuoga kwa shule kufurika!

February 20th, 2024 1 min read

NA WAANDISHI WETU

KUONGEZEKA kwa idadi ya wanafunzi waliosajiliwa katika shule za umma, kumeweka wanafunzi kwenye hatari za kiafya na usalama ambazo zimesababisha hata vifo, Taifa Leo inaweza kufichua.

Utafiti wa kote nchini unaonyesha kuwa shule nyingi zimekiuka miongozo ya afya na usalama iliyowekwa na Wizara ya Elimu kutokana na kukosekana kwa huduma za ukaguzi kutoka Idara ya Ubora katika Wizara.

Madarasa na mabweni yamejaa huku uhaba wa vifaa kama vyoo ukihatarisha afya za wanafunzi, tatizo ambalo limedhihirika zaidi katika makazi ya watu wenye kipato cha chini katika maeneo ya mijini.

Baadhi ya madarasa yana wanafunzi wapatao 200, zaidi ya 45 waliopendekezwa na Shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Elimu na Sayansi na Utamaduni (Unesco).

Msongamano huo umeathiri ufanikishaji wa mtaala na matokeo ya wanafunzi, na hivyo kurudisha nyuma mafanikio yaliyopatikana kufikia sasa katika kufaulisha elimu kwa wote.

Vifaa vya usafi wa mazingira ni haba huku visa vya utovu wa nidhamu pia vikitokea kwa sababu ni vigumu kuwasimamia wanafunzi wengi bila wafanyakazi wa kutosha.

Wakati wa mapumziko, wanafunzi hulazimika kupanga foleni kwenye mabafu machache huku ikichukua baadhi yao hata wiki moja kupata nafasi ya kuoga.