Habari za Kitaifa

Wazazi wahimizwa kupeleka watoto wao kukaguliwa Saratani

Na LAWRENCE ONGARO September 15th, 2024 1 min read

WAZAZI wamehimizwa kupeleka watoto wao wafanyiwe ukaguzi wa Saratani, ili kubaini hali yao ya afya mapema.

Himizo hilo lilitolewa Ijumaa wiki jana na Mkurugenzi Mkuu wa Afya nchini Patrick Amoth, alipozuru Hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Chuo Kikuu cha Kenyatta (KUTRH).

Taasisi hiyo tayari imetenga wadi mahsusi kutibu watoto wenye aina kadha za Kansa.

Kwa muda wa mwaka moja sasa hospitali hiyo imekuwa ikihudumia wagonjwa wa Saratani wapatao 50 ambapo wawili wametibiwa na kupona.

“Chuo Kikuu cha Manchester kimeweka ushirikiano wa karibu na hospitali ya KUTRH, ili kuboresha masuala ya utafiti wa Saratani. Hii ni habari njema na hivyo wazazi wanafaa kuleta watoto wao wenye matatizo hayo katika KUTRH ili wafanyiwe ukaguzi na kutibiwa,” Dkt Amoth akasema.

Alisema kila mwaka visa 3,000 vipya vya Saratani huripotiwa humu nchini.