• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 AM
Simbas yaanza kujipanga kwa mchujo kufuzu kwa Kombe la Dunia

Simbas yaanza kujipanga kwa mchujo kufuzu kwa Kombe la Dunia

Na GEOFFREY ANENE 

KENYA Simbas itarejelea mazoezi yake Septemba 3 kujiandaa kwa mchujo wa mwisho wa kufuzu kushiriki Kombe la Dunia la raga ya wachezaji 15 kila upande mwaka 2019 utakaoandaliwa kutoka Novemba 11-23, 2018 mjini Marseille, Ufaransa.

Simbas ya kocha Ian Snook ilipoteza nafasi ya kufuzu moja kwa moja kupitia mchujo wa Bara Afrika iliponyukwa 53-28 na Namibia katika fainali ya Kombe la Afrika la Dhahabu jijini Windhoek mnamo Agosti 18.

Mabingwa wa Afrika mwaka 2011 na 2013, Kenya, watakabana koo na Canada (Novemba 11), Hong Kong (Novemba 17) na Ujerumani (Novemba 23) katika mchujo wa mwisho ambao mshindi atajikatia tiketi ya kumenyana na New Zealand, Afrika Kusini, Italia na Namibia katika Kundi B la Kombe la Dunia.

Kenya haijawahi kukutana na Canada katika historia yake. Inafahamu Ujerumani na Hong Kong.

Ikinolewa na raia wa Afrika Kusini Jerome Paarwater, Kenya ililimwa 30-29 na Ujerumani katika mechi ya kirafiki mnamo Mei 27 mwaka 2017 uwanjani RFUEA jijini Nairobi.

Imekabiliana na Hong Kong mara sita. Simbas ilipepetwa 44-17 zilipokutana mara ya kwanza kabisa katika shindano la mwaliko mnamo Desemba 13 mwaka 2011 mjini Dubai nchini Milki za Kiarabu. Kenya kisha ilizaba Hong Kong 24-18 na 34-10 jijini Nairobi mwaka 2016. Mwaka 2017, Kenya ilikaba Hong Kong 19-19 Agosti 20 na kulimwa 43-34 Agosti 26 jijini Nairobi katika mechi za kirafiki uwanjani RFUEA kabla ya kulemewa tena 40-30 Novemba 17 mjini Hong Kong katika shindano la Cup of Nations.

Katika viwango bora vya raga duniani vya wakati huu, Hong Kong, Canada, Kenya na Ujerumani zinashikilia nafasi za 21, 23, 28 na 29, mtawalia.

Ratiba na matokeo ya Simbas mwaka 2018:

Novemba 11

Canada na Kenya (6.30pm)

Novemba 17

Hong Kong na Kenya (4.00pm)

Novemba 23

Kenya na Ujerumani (8.00pm)

Juni 23

Morocco 24-28 Kenya

Juni 30

Kenya 45-36 Zimbabwe

Julai 7

Kenya 38-22 Uganda

Agosti 11

Kenya na Tunisia

Agosti 18

Namibia 53-28 Kenya

You can share this post!

Kesi ya Mwilu yaibua kero la uchaguzi 2017

Roho mkononi Gor ikimenyana na USM Alger

adminleo