‘Sultan’ Joho aponyoka kesi ya maadili
WAZIRI wa Madini, Hassan Ali Joho amepata afueni baada ya Mahakama Kuu kutupilia mbali ombi la kutaka atangazwe kuwa hafai kushikilia wadhifa wa umma kutokana na madai ya kutotii amri ya mahakama alipokuwa Gavana wa Mombasa.
Kesi hiyo iliwasilishwa na wafanyabiashara Ashok Labshanker Doshi na Pratibha Ashok Doshi baada ya Bw Joho kupatikana na hatia ya kudharau amri ya mahakama na kuhukumiwa mwaka 2021.
Doshi walitaka mahakama itamke kuwa Bw Joho alikiuka masharti ya Katiba kuhusu uongozi na uadilifu na kumzuia kabisa kushikilia wadhifa wowote wa umma au Serikali.
Mzozo huo ulitokana na kesi ya ardhi kuhusu kipande cha ardhi cha ekari mbili huko Changamwe.
Mnamo Mei 2019, maafisa wa Kaunti ya Mombasa wakiongozwa na Bw Joho walibomoa ukuta wa uzio uliokuwa kwenye ardhi hiyo iliyokuwa na mgogoro.
Serikali ya Kaunti ilidai kuwa ardhi hiyo ilikuwa mali ya shule ya eneo hilo, huku akina Doshi wakisisitiza kuwa ilikuwa mali yao binafsi na ilikuwa imelindwa na amri ya mahakama.
Ubomoaji huo ulizua mzozo , ambapo Mahakama ya Mazingira na Ardhi mnamo Februari 12, 2020, ilimpata Bw Joho na hatia ya kutotii amri ya mahakama.