• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 3:25 PM
Wasomi nchini kutathmini kama ICC ni muhimu kwa Kenya

Wasomi nchini kutathmini kama ICC ni muhimu kwa Kenya

NA LAWRENCE ONGARO

WASOMI wa kisheria nchini wanapanga kuchapisha kitabu kitakachochanganua kwa undani kuhusu kama Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) ni muhimu kwa Kenya.

Kwenye kongamano la siku mbili lililofanyika katika Chuo cha Kenyatta kujadili kuhusu utenda kazi wa Mahakama ya kimataifa ya ICC, wasomi mbalimbali walitoa maoni yao kuhusu mahakama hiyo ambayo imekuwa ikikashifiwa vikali na viongozi wa Afrika

Miaka 20 imepita tangu kutiwa saini mkataba wa Roma ulioasisi Mahakama ya ICC na kongamano hilo lilikuwa kati ya shughuli nyinginezo zinazoendelezwa kimataifa kwa maadhimisho ya kuanzishwa kwake.

Msomi wa kisheria Profesa Makau Mutua alisema mahakama hiyo inastahili kuwepo lakini isiwe ikibagua kwa kuwashtaki Waafrika pekee.

Aliongeza kuwa mahakama hiyo inastahili kupata mamlaka zaidi ili kutekeleza wajibu wake ipasavyo.

“Waathiriwa wengi huachwa wakisononeka kwa sababu washukiwa wengi hawapewi adhabu inayostahili,” alisema Profesa Mutua.

Ilidaiwa kuwa lawama chungu nzima zinazolimbikiziwa ICC zimeponza juhudi zake za kutekeleza majukumu yake kikamilifu.

Wakili Mkuu wa Serikali, Bw Kenneth Ogetto aliyemwakilisha mwanasheria mkuu Bw Kihara Kariuki, alisema ni muhimu kutathmini kwa kina umuhimu wa mahakama hiyo.

Humu nchini, majukumu ya mahakama hiyo yalizua ubishi mkubwa baada ya Rais Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto kulazimika kuwa kizimbani wakifuatilia kesi za ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007.

Bw Ogetoalitoa mfano wa John Bolton, ambaye ndiye mkuu wa kiusalama nchini Marekani ambaye ambaye hivi majuzi alikosoa mahakama ya ICC kuhusu utenda kazi wake inapoendeleza uchunguzi kuhusu matukio ya ghasia Afghanistan ambako wanajeshi wa Amerika walihusika pakubwa.

Kwa kauli moja wasomi waliohudhuria walikubaliana kuchapisha kitabu kitakacho angazia maswala muhimu ya ICC.

You can share this post!

Watoto waliofariki Pumwani kufanyiwa upasuaji

Aliyemuua nyanyake na kuhepa asakwa

adminleo