• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 3:25 PM
NGILA: Safari za moja kwa moja hadi Amerika ziimarishe utalii nchini

NGILA: Safari za moja kwa moja hadi Amerika ziimarishe utalii nchini

NA FAUSTINE NGILA

MAENDELEO ambayo yameshuhudiwa katika sekta ya utalii mwezi Oktoba yanastahili pongezi. Wakati nilihudhuria kikao cha pamoja kati ya Wizara ya Utalii na kampuni ya Google mtaani Westlands, Nairobi, nilijionea juhudi za hakika za kuimarisha utalii nchini.

Waziri Najib Balala aliishukuru Google kwa kuzindua huduma ya Street View ambapo watalii watajionea mandhari ya mbuga zetu kwa simu zao popote walipo duniani, kabla ya kuzuru humu nchini.

Na hapo jana, ndege ya kwanza ya safari ya moja kwa moja kutoka Kenya ilitua nchini Amerika katika mchakato uliochukua miongo sita na kuifanya nchi hii kuwa ya kwanza Afrika Mashariki kujivunia huduma hiyo ya kipekee.

Na sasa serikali inalenga kuvutia watalii zaidi ya 2.5 milioni kila mwaka kufikia mwaka 2022. Idadi hii inamaanisha utalii nchini utakua kwa asilimia 72 kutoka kwa watalii 1.14 milioni ambao walifika nchini 2017.

Si siri tena kwamba utalii wa Kenya kwa sasa uko katika hali nzuri. Kulingana na Baraza la Kimataifa la Utalii na Safari, utalii wetu unachangia asilimia 15.2 ya mauzo yote katika mataifa ya kigeni na asilimia 8.9 ya ajira.

Ninatumai kuwa hata wakati serikali inaonyesha jitihada zake katika kuimarisha sekta hii, haitasahau changamoto zinazotishia kuyumbisha uchumi wetu.

Tunajua fika kuwa usalama ni nguzo muhimu ya kuvutia raia wa nchi za kigeni kuzuru mbuga zetu. Hivyo basi, wanajeshi wetu wanafaa kuilinda mipaka ya Kenya dhidi ya uvamizi huku pia wakizuia utovu wa usalama humu nchini.

Utegemezi

Wakati sasa umefika kwa serikali kukoma kutegemea watalii kutoka nje ya nchi. Inafaa kuzidisha juhudi za kuwahamasisha Wakenya kuzuru taifa lao wenyewe na miundombinu iwekwe.

Bila hili, tutazidi kukumbana na hali ngumu katika sekta hii wakati ambapo mataifa ya kigeni yanawashauri raia wake dhidi ya kusafiri kuja Kenya.

Pia, iwapo kampuni yetu ya ndege ya Kenya Airways inalenga kuvuna vizuri kutokana na safari za moja kwa moja hadi jijini New York, basi inafaa kuhakikisha nauli yake haizidi ile ya kampuni shindani za ndege.

Itakuwa aibu kwa watalii kuondoka nchini Kenya wakielekea Amerika, au Amerika wakija nchini kwa kampuni pinzani za ndege kutokana na sababu kuwa eti nauli za Kenya Airways ni ghali mno.

Kauli mbiu ya kampuni hiyo ni ‘Fahari ya Afrika.’ Inafaa kukuza imani katika kaulimbiu yake kupitia kwa utendakazi wake wa kuvutia watalii wa bara hili.

You can share this post!

Buda mlevi achoma mtoto kwa uji moto

TAHARIRI: Wanaotuongoza wawe wamesoma

adminleo