• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 4:55 PM
TAHARIRI: Vita dhidi ya ufisadi havilengi kabila lolote

TAHARIRI: Vita dhidi ya ufisadi havilengi kabila lolote

NA MHARIRI

Madai yaliyotolewa na baadhi ya viongozi wa kisiasa kutoka eneo la Bnde la Ufa kwamba vita dhidi ya ufisadi vinavyoendelea humu nchini vinalenga watu kutoka jamii fulani yanafaa kushutumiwa vikali.

Madai hayo ambayo yalitolewa na Seneta wa Nandi Samson Cherargei (pichani) kwamba maafisa wanaosimamia mashirika na taasisi mbalimbali kutoka Bonde la Ufa wanalengwa katika vita hivyo yanatishia kurejesha nyuma hatua ambazo Kenya imepiga katika kuangamiza zimwi la ufisadi.

Kulingana na Bw Cherargei, vita hivyo vinalenga kusambaratisha azma ya Naibu wa Rais William Ruto kuingia Ikulu 2022.

Lakini Naibu wa Rais amekuwa akikariri kuwa wanaolengwa ni wafisadi na wala si watumishi wa umma wasio na hatia.

Je, Seneta Cherargei anazungumza kwa niaba ya nani, ikiwa hata Bw Ruto hakubaliani na madai yake?

Tumekuwa tukiona watu kutoka maeneo mbalimbali wakikamatwa tangu kuanza kwa vita vya ufisadi humu nchini. Hivyo madai kwamba vita hivyo vinalenga watu wa jamii moja si ya kweli.

Kulingana na ripoti mbalimbali ambazo zimewahi kutolewa, nchi hii hupoteza zaidi ya nusu ya fedha za bajeti yake kwa wafisadi.

Mathalan, aliyekuwa mwenyekiti wa Tume ya Maadili na Kukabiliana na Ufisadi (EACC), Philip Kinisu alifichua kuwa Kenya hupoteza Sh608 bilioni katika ufisadi.

Kuingiza siasa katika vita dhidi ya ufisadi kunamaanisha kuwa wanasiasa hao wanataka fedha hizo ziendelee kuishia katika mifuko ya watu wachache huku mlipa-ushuru akiendelea kuteseka kutokana na gharama ya juu ya maisha.

Kulingana na takwimu za EACC, zaidi ya faili 180 za washukiwa waliochunguzwa katika mwaka wa matumizi ya fedha wa 2017/18 uliokamilika Juni 30, mwaka huu, tayari zimepelekwa katika afisi ya Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka ya Umma (DPP) ili hatua zaidi ziweze kuchukuliwa.

Takwimu hizo pia zinaonyesha kuwa EACC ilipokea malalamishi zaidi ya 400 na 150 kati yazo zimefanyiwa uchunguzi na wahusika kuchukuliwa hatua.

Je, washukiwa hao wote wanatoka katika jamii moja? Wanasiasa wanafaa kuweka kando masiahi yao ya kibinafsi na badala yake kuunga mkono juhudi za serikali kukabiliana na jinamizi la ufisadi.

You can share this post!

OBARA: Jopo la kuchunguza makosa vitabuni liokoe watoto...

La Liga ilivyopoteza ladha bila ya Neymar, Ronaldo kwa...

adminleo