• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 3:53 PM
MWAKA MPYA 2019: Wito wa amani na umoja Kenya

MWAKA MPYA 2019: Wito wa amani na umoja Kenya

BENSON MATHEKA na BRIAN OCHARO

WAKENYA wamehimizwa kuishi kwa umoja na amani mwaka huu ili nchi ipate ustawi wa kiuchumi.

Viongozi wa mirengo yote ya kisiasa na kidini walitoa wito kwa Wakenya kukumbatia undugu na kuungana ili kustawisha nchi yao 2019. Akiwa Mombasa, Rais Uhuru Kenyatta aliwataka Wakenya kuishi kama ndugu na kuheshimiana.

“Sisi ni familia moja ya watu wa Kenya na taifa la Kenya. Tunapaswa kujifunza kuishi, kufanyakazi pamoja na kuheshimu kila mmoja kwa lengo la kujenga nchi yetu,” alisema.

Kiongozi wa chama cha ODM, Raila Odinga, alisema ana matumaini kwamba mwaka wa 2019 utakuwa wa ustawi nchini. “Ninajiunga nanyi Wakenya wenzangu katika matumaini yenu na kuwatakia mwaka wa 2019 wenye ustawi. Ingawa 2018 ulianza kwa hali ngumu, tuliumaliza kwa matumaini. Niko na hakika siku zijazo zitakuwa bora zaidi kwetu,” alisema Bw Odinga kwenye risala ya mwaka mpya.

Aliwakumbusha Wakenya kwamba, walimaliza mwaka wa 2018 kwa utulivu kwa sababu ya kuchagua amani.

“Kama kuna kitu tulichojifunza 2018 ni kwamba, watu huwa kile wanachochagua kuwa. Tunaweza kuchagua kugawanya au kuunganisha nchi, kupigana wenyewe kwa wenyewe kwa misingi ya kikabila au kuungana kama jamii moja iliyo na mwelekeo mmoja, tunaweza kuungana kupigana na ufisadi na kuepuka adhabu au kukubali maovu haya ambayo yametuangamiza kwa muda mrefu,” alisema Bw Odinga.

“Ninajitolea kuendelea na chaguo nzuri za 2018 na kufanya chaguo sawa mradi tu ni kupeleka Kenya na Afrika mbele 2019,” akaongeza.

Kwenye risala yake, Rais mstaafu Daniel Moi aliwataka Wakenya kukumbatia amani na umoja. “2019 uwe mwaka wa amani na umoja wa taifa,” alisema na kuongeza kuwa nchi haiwezi kupata maendeleo ya kiuchumi ikiwa imegawanyika.

Kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka alisema 2019 utakuwa mwaka wa mabadiliko makubwa kwa maisha ya Wakenya chini ya muafaka wa viongozi wa serikali na upinzani. Katika risala yake ya mwaka mpya, mwenyekiti wa chama cha Kanu aliye pia Seneta wa Baringo, Gideon Moi aliwataka Wakenya kuishi kama watu wa taifa moja.

Gavana wa Mandera Ali Roba alitoa wito kwa Wakenya kutetea na kulinda ugatuzi mwaka huu mpya wa 2019. Kwenye taarifa, Bw Roba ambaye ni mwenyekiti wa baraza la maendeleo la kaunti za kaskazini mwa Kenya aliunga marekebisho ya katiba lakini akasema yanafaa kushirikisha maslahi ya Wakenya wote.

Alisema ugatuzi umesaidia kubadilisha nchi na unafaa kulindwa. “Ni matumaini yangu kwamba ugatuzi utatiwa nguvu zaidi na kulindwa na wote,” alisema Bw Roba.

Viongozi wa dini ya Kiislamu eneo la Pwani nao waliwaomba Wakenya kuhubiri amani wanapoendelea na sherehe za mwaka mpya wa 2019. Wakiongozwa na Katibu Mwandalizi wa Baraza la Waislamu na Wahubiri wa Kenya, Sheikh Mohamed Khalifa, waliwaomba wanasiasa kuepuka siasa za ukabila na kuunganisha Wakenya ili kuwe na maendeleo nchini.

You can share this post!

DCI azimwa kumchunguza Prof Ojienda

2022: Ruto hahitaji tiketi ya moja kwa moja ya Jubilee,...

adminleo