• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 6:27 PM
KANU yamkemea Ruto kubadili nia kuhusu katiba

KANU yamkemea Ruto kubadili nia kuhusu katiba

Na WYCLIFF KIPSANG

VIONGOZI wa Chama cha KANU wamemkashifu Naibu Rais William Ruto kwa kupinga kura ya maamuzi ambayo itapelekea kupunguza idadi ya kaunti na madiwani.

Katibu Mkuu wa chama hicho, Bw Nick Salat, jana alisema naibu rais anafaa awe anasaidia taifa kupunguza gharama ya kulipa mishahara ya watumishi wa umma.

“Inaonekana hajali kuhusu Kenya. Anamaanisha tuendelee kuwa na wafanyakazi wengi shambani wanaozalisha mazao machache, au tupunguze idadi hiyo? Inafaa azingatie hali ya kifedha ya nchi hii,” akasema Bw Salat.

Aliongeza: “Ninashangaa kuona naibu rais akitetea gharama kubwa ya mishahara ambayo haiwezi kustahimiliwa na mapato yetu ya jumla ya taifa. Tunahitaji kupunguza gharama ya mishahara ikiwemo kwa kupunguza idadi ya wafanyakazi.”

Viongozi wa KANU pia walimkosoa kwa kudai kwamba rekodi yake ya maendeleo inaonyesha wazi uwezo wake wa uongozi na hahitaji kushikwa mkono na vigogo wa kisiasa ndipo ashinde urais 2022.

Mwenyekiti wa chama hicho, tawi la Kaskazini mwa Rift Valley, Bw Paul Kibet, alisema miradi ambayo Bw Ruto amekuwa akizindua maeneo mbalimbali nchini haina msingi kwani ni miradi inayotekelezwa na wabunge katika maeneobunge yao.

“Kile anachofanya ni kuharibu fedha za umma kwa kazi ambazo zinaweza kushughulikiwa hata na wasimamizi wa kaunti ndogo. Ana kipi kipya anachoweza kutuonyesha ilhali watu wake wanakumbwa na umaskini? Badala ya kujitahidi kuinua hali ya maisha kwa wananchi, anawaambia waanze kilimo cha parachichi ambayo haiwezi kuwasaidia kiriziki,” akasema Bw Kibet.

Hivi majuzi, Naibu Rais alisema ataunga mkono marekebisho ya katiba ikiwa tu yatahusu kuimarisha ugatuzi.

Wakati Dkt Ruto alipokutana na madiwani wa Kaunti za Kakamega, Baringo na Elgeyo-Marakwet bomani mwake Sugoi, Kaunti ya Uasin Gishu, alisisitiza ataunga mkono mjadala wowote utakaohusu tu uimarishaji wa ugatuzi na kuongeza mgao wa fedha kwa serikali za kaunti wala si kubuni nafasi za kisiasa kwa manufaa ya viongozi wachache.

“Kinyume na inavyodhaniwa, sipingi marekebisho ya katiba. Kitu chochote kitakachoathiri matunda ya ugatuzi ndicho kitapingwa. Tunataka kuona marekebisho ambayo yatawezesha kaunti kustawi,” akasema Dkt Ruto.

Kulingana naye, hakuna jinsi wapinzani wake wanaomezea mate urais 2022 watamshinda kwa kusubiri kupigiwa debe na vigogo wengine wa kisiasa kama hawana miradi ya maendeleo wanayoweza kuonyesha wananchi.

“Kuna wale wanaosubiri kutangazwa kuwa wanatosha. Unatarajiaje kupigiwa debe kama huna ajenda wala mpango utakaonufaisha nchi?” akauliza Ruto.

“Niko tayari kupambana na mtu yeyote. Acha wapinzani wangu waonyeshe kile walichofanyia nchi hii,” akasema Naibu Rais ambaye pia alikuwa na viongozi wa Magharibi mwa Kenya.

Alisema mtu yeyote anayetaka kushindana naye uchaguzini yuko huru kwani haogopi ushindani.

You can share this post!

Makurutu wasimulia walivyohongana kuingia KDF

Prof Kibwana atakiwa kuomba msamaha kwa kumkejeli Kalonzo

adminleo