• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
Aukot awarai Wakenya kuunga mkono kampeni ya #PunguzaMzigo

Aukot awarai Wakenya kuunga mkono kampeni ya #PunguzaMzigo

Na CHARLES WASONGA

KIONGOZI wa Chama cha ThirdWay Alliance Ekuru Aukot amewataka Wakenya kuungana mkono mchakato wa marekebisho ya katiba unaopigiwa debe na chama hicho, akisema unalenga kuhakikisha kuwa pesa za umma zinagatuliwa hadi ngazi ya wadi.

Alisema kampeni yake maarufu kama “Punguza Mzigo Punda Amechoka” kufikia Jumanne asubuhi ilikuwa imepata sahihi 800,000 za Wakenya.

“Tunataraji kuwa ifikiapo Machi mwaka huu tutaweza kupata sahihi 200,00 zinazosalia ili kufikisha sahihi 1 milioni zinazohitajika kwa mujibu wa Katiba kufanikisha mpango huu. Tunawataka wananchi wengi kuunga mkono mchakato huu kwa sababu unalenga kuondoa viti mbalimbali vya uwakilishi ili pesa nyingi zielekezwe katika miradi ya afya, elimu, barabara, kati ya mingine,” Bw Aukot akawaambia wanahabari Jumanne katika makao makuu ya chama chake mtaani Lavington, Nairobi.

Alisema marekebisho ya katiba yanayopigiwa debe ya vyama vya ODM, Ford Kenya, KANU, na ANC yanalenga kuwaongeza Wakenya mzigo kupitia kubuniwa kwa nyadhifa zaidi ya uongozi kama vile cheo cha Waziri Mkuu na manaibu wake.

“Wakenya hawafai kuhadai na watu kama hawa ambao, walifaidi katika eneo ya utawala wa chama cha Kanu, lakini sasa wanawahadaa kwamba wanapigania marekebisho ya katiba. Huu ni unafiki uliokithiri mipaka,” akasema Bw Aukot.

Wakati huo huo, Bw Aukot amewasuta viongozi wa Jubilee kwa kuendeleza siasa za urithi wakati huu ambapo Wakenya wanawatarajiwa kutimiza zile ahadi ambazo walitoa wakati wa kampeni kuelekea uchaguzi mkuu wa Agosti 8, 2017.

“Inasitika kuwa vinara wakuu wa Jubilee wameanza kuzozana kuhusu siasa za 2022 ilhali hawatimiza ahadi ambazo waliwapa Wakenya. Sekta ya elimu inakabiliwa na changamoto, gharama ya maisha imepanda,vijana hawana ajira na wizi wa pesa za umma unaendelea katika idara zote za serikali ihali kile ambacho ngoma inayochezwa ni ile ya uchaguzi wa 2022,” akasema.

Bw Aukot akaongeza: “Ikiwa walianza kampeni za 2022, siku chache baada ya uchaguzi mkuu wa 2017 ina maana ahadi zote walizowapa Wakenya hazikuwa na maana yoyote. Waliwadanga wananchi ambao walijitokeza kwa wingi kuwapigia kura.”

Alimtaka Rais Uhuru Kenyatta kuwa mstari wa mbele kupalilia maridhiano ya kisiasa kwa kukoma kutumia maneno makali dhidi ya wanasiasa ambao wanahoji uongozi wake.

“Yeye ni kiongozi wa taifa na anapaswa kudhihirisha uvumilivu. Hafai kuwazomea viongozi wengine hadharani kwa maneno makali,” akasema Bw Aukot.

Mnamo Jumatatu, Rais Kenyatta aliwataja kama “washenzi” wanasiasa kutoka eneo la Mlima Kenya ambao wamekuwa wakidai kuwa serikali yake imetenga eneo hilo kimaendeleo.

“Wajibu wangu kama Rais ni kutahakikisha kuwa maendeleo yanasambazwa katika pembe zote nchini. Kuanza sasa nitazunguka kuanza Kisumu hadi Mombasa, Namanga hadi Lodwar kuzindua miradi ya maendeleo. Hizi siasa za kutaka maendeleo yakite katika eneo ambako kiongozi anatoka pekee sharti zikome,” akasema.

You can share this post!

Matiangi azima ‘Disco Matanga’ Kilifi kupunguza...

Mzozo ndani ya Jubilee ni hatari kwa muafaka, mashirika...

adminleo