Habari za Kitaifa

Ruto: Nitarejelea uinjilisti nikimaliza kuwa Rais

September 2nd, 2024 1 min read

RAIS William Ruto amedokeza kuwa atarejelea uinjilisti baada ya kustaafu wadhifa wa Rais wa tano wa Kenya.

Dkt Ruto alisema uinjilisti ndio ulikuwa ‘mwito’ wake wa kwanza kabla ya kujitosa katika siasa kwani alilelewa kupitia mafunzo ya neno la Mungu.

“Mimi ni mwinjilisti na nyakati zingine watu hushangaa kwa nini mimi husimama kwenye majukwaa hata juu ya magari. Ikiwa wewe ni mwinjilisti, nyakati nyingi huwa unadhihirisha tabia za mwinjilisti hata unapofanya mambo mengine,” Rais Ruto akasema.

Alikuwa akiongea Septemba 1, 2024 alipohudhuria ibada ya Jumapili katika Kanisa la Kianglikana la ACK, Cathedral mjini Bungoma.

Alisema mwenendo wake wa kuwahutubia waumini katika madhabahu na paa za magari, akisema hiyo inatokana na “mafundisho yake ya uinjilisti.”

“Nimeamua kwamba nikistaafu kama Rais nitarejelea kazi ya uinjilisti kwa sababu hiyo ndio mwito wangu asilia,” Dkt Ruto akasema.

Rais vile vile aliwataka viongozi wa makanisa kuendelea kuiombea taifa anapoendelea kung’ang’ana kukarabati uchumi wa Kenya.