Mapambano bado, wasema mashujaa wa Saba Saba
MIAKA 36 baada ya maandamano ya kihistoria ya Saba Saba ya Julai 7, 1990, baadhi ya viongozi walioongoza mapambano ya kurejesha mfumo wa vyama vingi vya kisiasa wanasema safari ya kupigania utawala bora bado haijakamilika.
Viongozi hao walikumbuka jinsi walivyokabiliana na ukandamizaji wa utawala wa aliyekuwa Rais Daniel arap Moi, huku wakisema hali iliyoshuhudiwa Jumanne ya kufungwa kwa barabara na kumwagwa kwa polisi wengi mijini iliwakumbusha matukio ya miaka hiyo.
Katika Saba Saba ya kwanza, serikali ya Moi ilizuia mkutano uliokuwa umeitishwa katika Uwanja wa Kamukunji, Nairobi na viongozi Kenneth Matiba na Charles Rubia.
Kabla ya mkutano huo, Matiba, Rubia na Raila Odinga walikamatwa na kuzuiliwa, lakini wanaharakati waliendelea na maandamano licha ya msako mkali wa vitengo vya usalama.
Shinikizo lililotokana na maandamano hayo lilichangia kufutwa kwa Kifungu cha 2A cha Katiba mwaka wa 1991 na kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi vya kisiasa.
Miongoni mwa waliokuwa mstari wa mbele katika mapambano haya walikuwa Odinga, James Orengo, Paul Muite, Gitobu Imanyara, Kiraitu Murungi, Njeru Kathangu, Mukhisa Kituyi, Martin Shikuku na Masinde Muliro, pamoja na viongozi wa kidini akiwemo Askofu Ndingi Mwana a’Nzeki, Mchungaji Timothy Njoya, Askofu David Gitari, Henry Okullu na Alexander Muge.
Gavana wa Siaya, Orengo, ambaye alijiunga na maadhimisho ya Saba Saba jijini Nairobi jana, alisema ni jambo la kusikitisha kuwa taifa hili bado halijatenga siku rasmi ya kuwaenzi mashujaa wa mapambano ya ukombozi wa pili.
“Kama ningekuwa rais chini ya Katiba hii mpya, ningetangaza Saba Saba kuwa siku ya kitaifa ya kuwaenzi watu kama Kenneth Matiba, Charles Rubia na Raila Odinga,” alisema.
Aliyekuwa mbunge wa Runyenjes, Kathangu, alisema kurejeshwa kwa vyama vingi hakukuleta mageuzi yote yaliyotarajiwa kwa sababu wengi wa wanaharakati walikuwa gerezani wakati vyama vipya viliposajiliwa.
“Tulitarajia Wakenya wapate viongozi wapya, lakini wengi wetu tulikuwa kizuizini. Vijana wa Gen Z wanapaswa kuendelea kupigania utawala bora kama tulivyofanya mwaka wa 1990,” alisema.
Kwa upande wake, wakili Muite alisema mapambano ya Saba Saba yalizaa matunda makubwa, ikiwemo Katiba ya mwaka wa 2010 ambayo imeimarisha haki na uhuru wa wananchi.
Alisema Wakenya, hasa vijana wa Gen-Z, wameonyesha ujasiri mkubwa wa kuwawajibisha viongozi na kusisitiza kuwa ukiukaji wa haki za binadamu lazima uwajibishwe watu.
Hata hivyo, kiongozi wa ODM, Oburu Oginga alisema Saba Saba haipaswi kuwa siku ya maandamano ya barabarani bali ya kutafakari mafanikio yaliyopatikana tangu kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi.
Naye Seneta wa Kitui, Enoch Wambua alisema Saba Saba inaendelea kuwa ukumbusho wa mapambano ya demokrasia na utawala bora, akiongeza kuwa vijana wa sasa wamechukua nafasi ya kizazi kilichopigania mageuzi miaka ya 1990 katika kudai uongozi wajibifu.