Habari za Kitaifa

IEBC yafufua mpango wa kupimia wanasiasa pesa za kampeni

Na EDWIN MUTAI July 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imefufua mpango wake wa kudhibiti matumizi ya fedha katika kampeni za uchaguzi kwa kuchapisha rasimu ya kanuni mpya zinazolenga kuweka kiasi cha matumizi ya wagombea na vyama vya kisiasa katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027.

Katika rasimu hiyo iliyochapishwa Jumatatu, Julai 6, 2026, IEBC imependekeza kuwa mgombea urais asitumie zaidi ya Sh4.44 bilioni katika kampeni zake, huku matumizi ya chama cha kisiasa yakipangwa kutozidi Sh17.7 bilioni.

Kwa mujibu wa mapendekezo hayo, wagombea wa ugavana, useneta na uwakilishi wa wanawake wataruhusiwa kutumia kati ya Sh12.3 milioni na Sh123 milioni, kutegemea ukubwa wa kaunti na idadi ya wakazi.

Wanaowania ubunge watatumia kati ya Sh17.5 milioni na Sh123 milioni, huku wanaowania uwakilishi wa wadi katika mabunge ya kaunti wakiruhusiwa kutumia kati ya Sh2.5 milioni na Sh20 milioni kulingana na ukubwa na idadi ya wakazi wa wadi husika.

Hii ni mara ya pili kwa IEBC kujaribu kudhibiti matumizi ya fedha za kampeni baada ya juhudi za mwaka 2016 kugonga mwamba.

Wakati huo, Bunge lilisitisha utekelezaji wa kanuni hizo kwa kurekebisha Sheria ya Ufadhili wa Kampeni za Uchaguzi na kuahirisha utekelezaji wake hadi baada ya uchaguzi wa mwaka 2017.

Uwajibikaji

Mwenyekiti wa IEBC Erastus Ethekon amesema kanuni hizo zinalenga kuimarisha uwajibikaji na uwazi katika usimamizi wa fedha za kampeni.

“Kanuni hizi zinakusudia kuimarisha uwajibikaji katika usimamizi wa fedha za kampeni za wagombeaji na vyama vya kisiasa,” alisema Bw Ethekon.

Alisema Sheria ya Ufadhili wa Kampeni za Uchaguzi ya mwaka 2013 inapatia IEBC mamlaka ya kuweka viwango vya michango, matumizi na kusimamia uwajibikaji wa fedha za kampeni.

IEBC pia imewapa Wakenya hadi Julai 15, 2026 kuwasilisha maoni yao kuhusu rasimu hiyo kabla ya kanuni hizo kuidhinishwa.

Wakati huo huo, tume hiyo imekumbusha wadau kuhusu ratiba ya maandalizi ya uchaguzi wa mwaka 2027.

Kwa mujibu wa ratiba hiyo, maafisa wa umma wanaonuia kugombea viti watalazimika kujiuzulu ifikapo Februari 9, 2027, miezi sita kabla ya uchaguzi.

Vyama vya kisiasa vitapaswa kuwasilisha orodha ya wanachama na majina ya wanaotaka kushiriki kura za mchujo ifikapo Machi 16, 2027, huku mchujo wa vyama ukitarajiwa kukamilika ifikapo Mei 9, 2027.

Uteuzi rasmi wa wagombea wa vyama na wawaniaji huru utafanyika kati ya Mei 29 na Juni 11, 2027, huku malalamishi yote yanayohusu uteuzi yakitakiwa kuwasilishwa kwa IEBC kabla ya Juni 12, 2027.

Hatua ya IEBC ya kupendekeza kiwango cha pesa za matumizi ya kampeni inajiri wakati ambapo wanasiasa wengi wamekuwa wakitumia mabilioni ya fedha katika shughuli za uwezeshaji wa wananchi, ambazo zimekuwa zikitafsiriwa kama kampeni za mapema kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.