• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
Tutapendekeza wanawake watengewe 50% ya nafasi za uongozi – Waiguru

Tutapendekeza wanawake watengewe 50% ya nafasi za uongozi – Waiguru

Na BERNARDINE MUTANU

GAVANA wa Kirinyaga Anne Waiguru Jumanne alisema viongozi wa kike watapendekeza kuondolewa kwa viti ‘maalum’ wakati wa kura ya maamuzi.

Akiwahutubia zaidi ya wasimamizi 300 wa wadi, kutoka kaunti zote 47, waliokuwa wamehudhuria mkutano wa siku tatu taasisi ya mafunzo ya kifedha (KSMS), Bi Waiguru alisema viongozi wa kike watatoa pendekezo la kugawana kwa asilimia 50-50 nafasi za uongozi nchini hasa kutokana na kuwa kanuni ya thuluthi mbili imekataa kufanya kazi.

Alisema, pendekezo hilo, ambalo watatoa wakati wa kura ya maamuzi ikiwa itafanyika, halina ‘nafasi maalum’ ambazo zitatolewa kwa wanawake wanaotafuta nafasi za uongozi.

“Tutatuma pendekezo la kishujaa ikiwa kutakuwa na kura ya maamuzi. Kanuni ya thuluthi mbili haifanyi kazi na tunapendekeza kugawana nafasi za uongozi kwa asilimia 50 -50,” alisema.

Gavana huyo alisema licha ya changamoto nyingi, uwakilishi wa wanawake nchini umeimarika na wanatarajia (wanawake) kupata magavana 10 wa kike 2022.

Hii ni kutokana na marekebisho ya kikatiba na utekelezaji unaoendelea wa usawa wa kijinsia na vile vile kujitolea kwa wanasiasa kuimarisha nafasi ya wanawake nchini.

Kwa sasa, kuna mawaziri sita wa kike, mawaziri wasaidizi wawili(CAS) kati ya 16 na makatibu wakuu nane kati ya 31.

“Siku za kesho zitakuwa nzuri na nafasi ya mwanamke itatambulika. Lakini wanafaa kuwa na uwezo wa kushindania nafasi katika sekta tofauti,” alisema, na kuwashauri wasimamizi hao kutwaa nafasi zilzoundwa na ugatuzi, Katiba, Agenda 4 za Maendeleo na mpango wa kujenga madaraja (BBI).

Aliwataka wasimamizi hao kufanya kazi na wasimamizi wa kaunti kwa lengo la kuwasaidia kukabiliana na changamoto za usimamizi. Aliongeza kuwa mkutano wa sita wa ugatuzi utaendeshwa Kirinyaga mnamo Machi 2019.

You can share this post!

Jagina Mkorea afa katika mbio za kilomita 10 Nyahururu

LAMU: Vijana kufadhiliwa baada ya kuhitimu masomo

adminleo