Shangazi Akujibu

Niliamua kula bata na binti mrembo sana, lakini nilichokumbana nacho…

October 28th, 2024 Kusoma ni dakika: 1

NIMEKUWA nikimchumbia huyu binti mrembo. Hivi majuzi, tuliamua kupeleka uhusiano wetu katika kiwango kingine ambapo tulishiriki mahaba. Lakini katika harakati hizo niligundua kwamba binti huyo anatoa uvundo katika sehemu ya uke. Simtaki tena.

Badala ya kumdharau jaribu kumsaidia ili apate matibabu kwani kuna uwezekano mkubwa kwamba harufu hiyo mbaya ni ishara ya matatizo ya kiafya. Pia wewe unapaswa ufanyiwe uchunguzi wa kimatibabu hasa ikiwa mlishiriki mahaba bila kinga.

Alipata ajali na sasa mahaba hayana utamu tena

Mke wangu alipata ajali miezi kadhaa iliyopita na katika harakati hizo kupoteza mguu wake mmoja. Nampenda lakini nahisi kwamba na ulemavu wake simtamani tena kimahaba. Nataka kuoa mke mwingine.

Ikiwa hajakukosea kwa nini utake kumuacha? Kumbuka kuwa dunia ni duara na kilichomfanyikia chaweza kukufanyikia pia. Ndoa inapaswa kuwa kwa uzuri au mabaya.

Mpango wa kando anataka nimuoe mke wa pili

Mimi ni mwanamume wa umri wa makamo na pamoja na mke wangu wa miaka 10 tumejaliwa watoto watatu. Kwa miezi kadhaa sasa nimekuwa na uhusiano wa pembeni na mwanamke mwingine ambaye amekataa kuniacha na anasema kwamba yuko tayari kuwa mke wangu wa pili. Nifanyeje?

Swali langu ni je uko tayari kupoteza ndoa yako kwa sababu ya mtu uliyekutana naye miezi michache iliyopita? Ikiwa jibu ni la basi wajua cha kufanya.

Nataka kumuacha kwa sababu ni bumbuazi kimasomo

Pamoja na mke wangu wa miaka mitano tuna watoto wawili. Nahisi kana kwamba hanifai kwa sababu mimi nimemaliza chuo na hata nina digrii mbili, ilhali yeye haonekani kutaka kujiendeleza kimasomo wala kitaaluma. Nimtemeje?

Unapaswa ujiulize kwa nini sasa ndio umeanza kuona kuwa mkeo ni mjinga? Badala ya kumdharau, pengine chukua muda wako kumsaidia ili pia naye ajiimarishe kimasomo na kitaaluma.