HabariHabari za Kitaifa

Tumechoka na ahadi hewa, tunataka kuona matunda ya kura zetu- Bunge la Mwananchi

Na WINNIE ONYANDO May 17th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

VUGUVUGU la Bunge la Mwananchi sasa linaitaka serikali ya Kenya Kwanza kuwajibika na kuacha kuendelea kutoa ahadi hewa.

Likiongozwa na rais wao Francis Awino, vuguvugu hilo linadai kuwa serikali ya Kenya kwanza ikiongozwa na Rais William Ruto inatoa ahadi baada ya ahadi bila kuzitimiza.

“Wakenya wamechoka kuambiwa, ‘tutafanya hili na lile’ bila kuona matunda. Huu sio muda wa kuzungumza maneno matupu. Wakenya wanataka kuona vitendo,” Bw Awino alisema Jumamosi Mai 17, 2025 alipokutana na wanabunge Jivanjee, Nairobi.

Kando na hayo, alitoa wito kwa vijana na wananchi kwa jumla kudai uwajibikaji, uwazi, na uongozi bora kutoka kwa serikali ya Kenya Kwanza, akisema kuwa taifa linapoteza mwelekeo kwa sababu ya uongozi mbaya.

Vuguvugu hilo pia lilikosoa mienendo ya kisiasa ya viongozi wa sasa, akisema kuwa wanajihusisha na kampeni za mapema badala ya kushughulikia matatizo yanayoikumba nchi, kama vile ukosefu wa ajira na gharama ya juu ya maisha.

“Katiba ya Kenya chini ya Kifungu cha 43 kinasema kuwa kila Mkenya ana haki ya kupata makazi bora, chakula, na huduma za afya. Lakini badala ya kuyatekeleza haya, serikali imejikita kwenye kampeni za mapema,” alisema Bw Awino.

Bw Awino pia alieleza wasiwasi wake kuhusu hatua za Rais Ruto, akidai kuwa amekuwa akijitangaza kama msemaji wa kisiasa wa maeneo mbalimbali kama vile Nyanza na eneo la Mlima Kenya badala ya kuunganisha taifa.

“Ni wakati wa kuangazia matatizo halisi yanayowakumba wananchi, sio maneno matupu ya kisiasa,” aliongeza.

Rais huyo wa Bunge la Mwananchi aliwahimiza vijana kushikilia msimamo thabiti na kushiriki kikamilifu katika mchakato wa mageuzi ya kijamii na kiuchumi, akisema huu ndio wakati wa “ukombozi wa tatu” wa Kenya.

“Wale wanaojihusisha na siasa kwa manufaa ya kibinafsi waendelee, lakini sisi vijana lazima tuwe macho kuiboresha na kuikomboa nchi yetu,” alisisitiza.

Kando na hayo, alitoa wito kwa wananchi wote kushirikirikiana ili kuiwajibisha serikali, akisema kuwa taifa bora linahitaji ushirikiano.

“Wakati wa mabadiliko umefika. Kenya iliyo na haki na usawa inawezekana ikiwa kila mmoja atatekeleza jukumu lake,” alisema.