Mwanaharakati Boniface Mwangi atimuliwa Tanzania, apatikana Ukunda
MWANAHARAKATI Boniface Mwangi, ambaye alikuwa akizuiliwa Tanzania amepatikana Ukunda, Kwale baada ya kutimuliwa katika nchi hiyo jirani.
Inasemekana aliondolewa nchini humo kurudishwa Kenya kwa barabara na kuachwa Ukunda.
Familia ya mwanaharakati huyo imethibitisha kuachiliwa kwake ikisema kuwa amekimbizwa hospitalini kwa uchunguzi.
Kutimuliwa kwake kunajiri saa chache baada ya serikali ya Tanzania kuwekewa presha kumwachilia huru.
Katibu wa Wizara ya Masuala ya Nje, Dkt Abraham Korir Sing’Oei, Alhamisi alilalamikia kutoweka kwa Bw Mwangi na akaiomba serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan kumtoa au kumwachilia.
“Wizara inabaini kuwa licha ya maombi kadhaa, maafisa wa serikali ya Kenya wamezuiwa kupata taarifa na pia kumfikia Bw Mwangi. Wizara pia ina wasiwasi kuhusu hali yake ya afya, ustawi wake kwa ujumla na ukosefu wa taarifa kuhusu kuzuiliwa kwake,” alisema Katibu huyo katika taarifa kwa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ya Tanzania.
Wanaharakati wa Kenya wameungana na serikali kulaani hatua ya serikali ya Tanzania kumkamata.
Hivi majuzi, Rais wa Tanzania alisema hataruhusu watu kutoka mataifa mengine kuleta vurugu nchini mwake.
“Tumeanza kuona mwenendo ambapo baadhi ya wanaharakati kutoka nchi jirani wanajaribu kuingilia mambo yetu. Kama wamekomeshwa kwao, basi wasije kuvuruga amani yetu hapa,” alisema Mama Suluhu.