Aroko aachiliwa huru tena kwa dhamana ya Sh0.3 milioni
MMOJA wa washukiwa wakuu katika mauaji ya Mbunge wa Kasipul Kabondo Charles Ong’ondo Were ameachiliwa kwa dhamana ya Sh300,000 pesa tasilimu.
Philip Aroko aliachiliwa na Jaji Diana Kavedza katika mahakama kuu ya Kibera.
Aroko aliachiliwa huru baada ya kukaa ndani siku saba polisi wakifanya uchunguzi.
“Upande wa mashtaka umekamilisha uchunguzi. Aroko ameshirikiana na polisi kukamilisha mahojianao yake nao,” kiongozi wa mashtaka alieleza Jaji Kavedza.
Aroko ni miongoni mwa washukiwa 11 waliotiwa nguvuni kuhojiwa kuhusiana na mauaji ya Were Aprili 30,2025.
Mshukiwa mkuu katika mauaji hayo Isaac Kuria Chege almaarufu Kush alikamatwa katika mji wa Isebania akijaribu kufuka mpaka kuingia nchini Tanzania alifikishwa katika mahakama iliyoko uwanja wa ndege wa Jomo Kenyatta.
Kuria amezuiliwa kwa siku 30 kusaidia polisi kukamilisha uchunguzi.
Kukamatwa kwa Kuria kumetisha watu 11 waliotiwa nguvuni kufuatia mauaji ya Were mnamo Aprili 30,2025.
Wengine wanaozuiliwa na polisi ni pamoja na dereva wake Allan Ogola Omondi pamoja na mlinzi wake Walter Owino Awino na jirani wake Kasipul, Ebel Ochieng almaarufu Dave Calo.
Ushahidi uliowasilishwa kortini umebaini kwamba Kuria alitiwa nguvuni katika hoteli moja Isebania.
Alikuwa na nduguye na kwamba alikuwa anajiandaa kuandamana na dada yake hadi Tanzania.
Hakimu mkazi mahakama ya uwanja wa ndege wa Jomo Kenyatta Irene Gichobi alielezwa na afisa anayechunguza kesi kwamba Kuria alitambuliwa kwa picha za video zilizomnasa akishuka kutoka kwa piki piki.
Mahakama iliambiwa mshukiwa alianza kumwandama Were kutoka bungeni hadi eneo la Mochari ya City alipoonekana akimfyatua risasi.
Alitoroka kwa piki piki.
Tangu siku hiyo alijificha hadi pale alipokamatwa Isebania.
Kesi hiyo itatajwa Juni 12, 2025.