Walioteuliwa IEBC wajitetea vikali bungeni
UKOSEFU wa imani kwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) katika kuendesha uchaguzi huru na haki ulitawala mchakato wa kuwahoji walioteuliwa kujiunga na tume hiyo.
Wabunge waliwahoji wagombea saba walioteuliwa kwa tume hiyo kuhusu jinsi, iwapo watapitishwa, watakavyorejesha imani ya Wakenya kwa tume hiyo kuhakikisha kila kura inahesabiwa.
Wanachama wa Kamati ya Haki na Masuala ya Sheria walioendesha mahojiano hayo walieleza kuwa Wakenya wengi wamepoteza imani na hawaamini uchaguzi utakuwa huru na wa haki.
Bw Erastus Ethekon, aliyeteuliwa kuwa mwenyekiti wa tume hiyo, alipata wakati mgumu kujibu maswali kuhusu kutopendelea upande wowote na uhusiano wake na serikali ya sasa. Bw Ethekon aliwahi kufanya kazi na aliyekuwa Gavana wa Turkana Josphat Nanok, ambaye kwa sasa ni Naibu Mkuu wa Wafanyakazi katika Ikulu.
Bw Ethekon alikiri kuwa alifanya kazi na Bw Nanok lakini alisisitiza kuwa uhusiano huo ulikuwa wa kikazi tu na uliisha mwaka wa 2022, na hautaathiri utendaji wake iwapo atateuliwa kuwa mwenyekiti wa IEBC.
Kwa upande wa Msajili wa Vyama vya Kisiasa Ann Nderitu, alikumbwa na madai kuwa alikwamisha usajili wa vyama vipya alipokuwa ofisini.
Bi Nderitu pia alikumbwa na madai kuwa uteuzi wake ulifanikishwa na “mkono wa mamlaka ya juu,” hali ambayo inaweza kuathiri kazi yake katika tume hiyo..
Hata hivyo, Bi Nderitu alijitetea dhidi ya madai hayo: “Sidhani kama kulikuwa na mkono wowote, kazi hizi zilikuwa wazi, niliomba kama Wakenya wengine. Simjui mtu yeyote.”
Bw. Moses Mukhwana, aliyeteuliwa kuwa kamishna, alikanusha madai ya kuwa karibu na Rais Ruto na Waziri Mkuu wa Kwanza Musalia Mudavadi.
Bw Mukhwana alikuwa wakili wa chama kilichovunjwa cha Amani National Congress (ANC) na aliteuliwa na Rais kuwa kwenye jopo la afya, jambo lililozua hofu kwa baadhi ya
Bi Mary Sorobit, aliyefanya kazi katika sekretarieti ya Jubilee kisha baadaye kujiunga na UDA ya Dkt Ruto, alijitetea dhidi ya madai kuwa atakuwa na upendeleo.
Aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Bonde la Ufa Hassan Noor alihojiwa kuhusu uhusiano wake na Kiongozi wa Wachache Bungeni Junet Mohamed na jinsi jina lake lilivyojumuishwa kwa kuchelewa.
Bw Noor alikiri kuwa yeye ni shemeji wa Bw Mohamed, jambo ambalo Mbunge Murugara alisema si tatizo kuwa na uhusiano wa kifamilia na mtu yeyote.