Habari za Kitaifa

GenZ aibuka na mbinu ya kuzuia wizi wa kura 2027 aliyojaribu katika uchaguzi wa Ol Kalou

Na KIMANI MWANGI July 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UCHAGUZI mdogo wa ubunge wa Ol Kalou ulilipa jukwaa la People’s IEBC funzo muhimu kuhusu changamoto za kutumia teknolojia katika kuthibitisha matokeo ya uchaguzi kwa wakati.

Jukwaa hilo, linaloendeshwa na vijana wenye ujuzi wa teknolojia, lilifanikiwa kuthibitisha matokeo kutoka vituo 93 kati ya 144 kabla ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kutangaza rasmi mshindi.

Hesabu zake zilionyesha mgombea wa DCP Sammy Ngotho akiwa mbele kwa asilimia 85.7 ya kura, akifuatiwa na mgombea wa UDA Samuel Muchina kwa asilimia 12.7.

Mwanzilishi wa teknolojia ya People’s IEBC, Daniel Miringa, alisema lengo halikuwa kuchukua nafasi ya IEBC bali kuonyesha kuwa wananchi wanaweza kutumia teknolojia kuthibitisha matokeo kwa uwazi.

Hata hivyo, mradi huo ulikumbana na changamoto kadhaa.

Baadhi ya waangalizi walishindwa kupata Fomu 35A baada ya polisi kutawanya watu kwa vitoza machozi na kuruhusu maafisa wa IEBC na maajenti wa vyama pekee kubaki ndani ya vituo vya kupigia kura.

Katika baadhi ya vituo, waangalizi walijiondoa dakika za mwisho kutokana na sababu binafsi, hali iliyolazimisha jukwaa hilo kusubiri IEBC kuchapisha fomu zilizokosekana ili kukamilisha hesabu zake.

Bw Miringa alisema ni muhimu kuwa na waangalizi wa akiba katika kila kituo cha kupigia kura ili kuhakikisha shughuli hiyo haiathiriki endapo mmoja atashindwa kutekeleza jukumu lake.

“Mbali na changamoto za nyanjani, mfumo huo pia ulikabiliwa na jaribio la udukuzi wa mtandao saa chache kabla ya uchaguzi kuanza.

“Kifaa kimoja kilituma zaidi ya maombi 200,000 kwa mfumo huo kwa lengo la kuulemea, lakini wahandisi walizuia majaribio hayo na mfumo ukaendelea kufanya kazi bila hitilafu,” akasema Bw Miringa.

Kutokana na tukio hilo, jukwaa hilo limeimarisha usalama wa mtandao kwa kuweka vizuizi dhidi ya maombi yasiyo ya kawaida ya udukuzi.

Baada ya majaribio ya Ol Kalou, People’s IEBC inapanga kushirikiana na mashirika yaliyoidhinishwa ya uangalizi wa uchaguzi kama ELOG pamoja na kutafuta idhini rasmi kutoka kwa IEBC ili waangalizi wake waruhusiwe kubaki vituoni hadi fomu za matokeo zitolewe.

“Wananchi wanastahili kuruhusiwa kupakua Fomu 35A moja kwa moja na kusambaza matokeo kupitia majukwaa mbalimbali ya kidijitali badala ya kutegemea TikTok pekee,” akaongeza.

Kwa mujibu wa Bw Miringa, uchaguzi wa Ol Kalou ulikuwa jaribio la kwanza la mfumo huo na umeonyesha kuwa teknolojia pekee haitoshi kuhakikisha uchaguzi huru na wa uwazi.

Alisema mafanikio yanategemea pia maandalizi mazuri, ushirikiano, ulinzi wa mtandao, upatikanaji wa vibali na imani ya wananchi.

Aliongeza kuwa mafunzo yaliyopatikana yataisaidia People’s IEBC kuboresha mfumo wake kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027 ili wananchi waweze kuthibitisha matokeo ya uchaguzi kwa uwazi zaidi.