Habari

Mwanaharakati wa ‘Reject Finance Bill’ aathiriwa na anemia akiwa kizuizini

Na KEVIN CHERUIYOT June 2nd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

FAMILIA ya Rose Njeri, mwanaharakati wa mitandaoni, aliyekamatwa kwa kuunda jukwaa la kutoa nafasi kwa Wakenya kutuma maoni ya kupinga Mswada wa Fedha wa 2025, imeelezea hofu kuhusu afya yake.

Bi Njeri, 35, aliyekamatwa na polisi Ijumaa katika mtaa wa South C, anakabiliwa na tuhuma za kuendeleza uhalifu mitandaoni kwa kuhimiza Wakenya kupinga mswada huo.

Sasa imeibuka kuwa Bi Njeri, mama wa watoto wawili, anaugua anemia inayosababishwa na ukosefu wa madini ya ‘iron’ mwilini.

Mama mzazi, Naombi Njoki, sasa anasema kuzuiliwa kwake kutaathiri kabisa afya yake na anataka polisi wamwachilie huru ili apate dawa.

“Naomba serikali imwachilie kwa sababu anao watoto wanaomtegemea na afya yake siyo nzuri. Amekuwa akiugua ugonjwa wa anemia na hali yake itazidi kuwa mbaya zaidi akiendelea kuzuiliwa,” Mama Njoki akasema baada ya kusafiri kutoka Nyeri baada ya kupata habari za kukamatwa kwa bintiye.

Akiongea na wanahabari jana nje ya Kituo cha Polisi cha Pangani, Nairobi, mama huyo alielezea kuwa bintiye hajatenda kosa lolote kuadhibiwa namna hiyo.

Naye Eva Waithera ambaye ni shangaziye Njeri alifichua kuwa baada ya kukutana naye siku mbili zilizopita, hali yake (Njeri) ya kiafya ilikuwa ikizorota na sasa anahofu kwamba hali yake itazorota zaidi.

“Hali yake ya afya siyo nzuri. Anahofia kilichomtendekea ikizingatiwa kuwa kuna baridi kali gerezani,” Bi Waithera akasema.

Bi Waithera alisema binti yao anahofia usalama wake ikizingatiwa kuwa polisi walitumia nguvu kupita kiasi walipomkamata.

“Hajui watu wanaozungumza naye. Unapoongea naye, unaona uwoga usoni mwake kwani anajaribu kuangalia kando kuona yule anayemwangalia,” Bi Waithera akaeleza.

Kundi la watetezi wa haki za kibinadamu walioungana na familia ya Njeri kushinikiza kuachiliwa kwake walidai kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) alitoa amri kwamba asiachiliwe huru hadi Jumanne wakati ambapo hatima yake itajulikana.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la kutetea haki la Vocal Africa Hussein Khalid na Boniface Mwangi waliwaongoza wanaharakati hao katika kuitaka serikali imwachilie huru Bi Njeri.

“Siyo hatia kwa Mkenya yoyote kuunda tovuti kufanikisha ukusanyaji maoni kutoka kwa umma. Walimkamata Ijumaa wakifahamu fika kuwa kuna wikiendi ndefu huku wakijua hana hatia. Hivi ni vitisho na njama ya kuwanyamazisha Wakenya, “ Bw Khalid akasema.

Mwanaharakati huyo ambaye ni miongoni mwa wale waliofurushwa kutoka Tanzania juzi aliisuta serikali ya Rais William Ruto kwa kukumbatia udikteta kupitia mbinu za kunyamazisha wakosoaji wake.