Habari

Umoja: Kalonzo ateua washirika wa Gachagua katika uongozi wa Wiper

August 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KIONGOZI wa Wiper Patriotic Front , Kalonzo Musyoka Ijumaa alitangaza mabadiliko katika uongozi wa chama hicho kwa kuwateua washirika wa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, huku akilenga kuonyesha umoja wa upinzani kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Bw Musyoka alimteua aliyekuwa waziri, Jamleck Kamau kuwa mwenyekiti wa chama, Mbunge wa Nyali, Mohamed Ali kuwa naibu kiongozi wa chama, na wakili wa masuala ya Katiba Ndegwa Njiru kuwa msemaji wa chama.

Uteuzi huo ulianza kutekelezwa mara moja na unaashiria upanuzi mkubwa wa uongozi wa Wiper vyama vya upinzani vinapoendelea na mashauriano kuhusu muungano w kukabiliana na Rais William Ruto mwaka 2027.

Bw Kamau, ambaye pia aliwahi kuwa Mbunge wa Kigumo, amewahi kuhusishwa kisiasa na Bw Gachagua, huku Bw Njiru akiwa mmoja wa mawakili mashuhuri waliowahi kumtetea kiongozi huyo wa DCP.

Bw Musyoka alisema uteuzi huo ulitokana na jukumu alilopewa na wajumbe wa chama wakati wa Kongamano la Kitaifa la Wajumbe la Oktoba 10 mwaka jana.

“Jukumu la kwanza nililopewa na wajumbe lilikuwa kutafuta urais wa Jamhuri ya Kenya mnamo Agosti 2027. Jukumu la pili lilikuwa kupanua na kujenga uongozi wa chama hiki hadi kiwe sura ya Kenya,” alisema.

Alisema mabadiliko hayo ni sehemu ya juhudi za kuimarisha Wiper pamoja na muungano mpana wa upinzani kuelekea uchaguzi wa 2027.

Bw Musyoka alisema mashauriano yanaendelea kuunganisha vyama vinavyopinga utawala wa Rais Ruto chini ya mwavuli mmoja wa kisiasa.

“Huu si uteuzi wa kujipendekeza, bali ni uteuzi wa imani. Kila mmoja wao anafaa kikamilifu katika chama ambacho ajenda yake pekee ni ‘Komboa Kenya’,” alisema.

Kando na mabadiliko hayo ya uongozi, Bw Musyoka alisema hataruhusu tofauti kati ya viongozi wa upinzani kuvuruga juhudi za kuunda muungano mmoja dhidi ya Rais Ruto.

Alisema viongozi wa upinzani wanaendelea na mashauriano ya kuleta pamoja Wakenya na akaonya kuwa mgawanyiko utawanufaisha viongozi wa Kenya Kwanza.

“Tunapoendelea na kazi hii, mashauriano yanaendelea ili kuleta upinzani chini ya mwavuli mmoja wa kuaminika. Tumekubaliana kuwa mgawanyiko ndiyo mkakati pekee wa utawala huu,” alisema.

Bw Musyoka pia aliwataka Wakenya kutotafsiri tofauti zinazojitokeza kati ya viongozi wa upinzani kama ishara kwamba mchakato wa kuunda muungano umevunjika.

“Hata mkiona tofauti kati ya viongozi wa vyama ndani ya muungano, tafadhali msizichukulie kwa uzito sana. Tumeungana kwa sababu tukigawanya upinzani, William Ruto atapata muhula wa pili,” alisema.

Alisema mashauriano yataendelea hadi vyama na viongozi wote wanaopinga serikali waungane.

“Mashauriano hayo yanaendelea na hayatasitishwa hadi kila chama na kila kiongozi anayepinga serikali awe chini ya paa moja, tayari kuunda serikali moja inayosubiri kuchukua uongozi,” alisema.