Huzuni tele watu 21 wafariki katika ajali barabarani ndani ya saa 24
WATU 21 wamepoteza maisha katika ajali tofauti za barabarani nchini ndani ya kipindi cha chini ya saa 24, hali inayozua wasiwasi kuhusu ongezeko la vifo vinavyotokana na ajali katika barabara kuu na maeneo hatari.
Ajali ya hivi punde ilitokea saa kumi na mbili alfajiri Jumamosi kwenye barabara ya Kimbimbi-Ngurubani, Kaunti ya Kirinyaga, ambapo watu wanane walifariki baada ya tuk-tuk kugongana na lori la kusafirisha mizigo.
Wengi wa waliofariki walikuwa vibarua waliokuwa wakielekea mashambani Mwea kupanda mpunga. Ajali hiyo ilitokea katika kijiji cha Murubara, eneobunge la Mwea Mashariki.
Nguvu ya mgongano iliharibu kabisa tuk-tuk hiyo na kuwanasa waliokuwa ndani. Waokoaji walitumia mashine maalumu kukata mabaki ya chuma ili kutoa miili huku jamaa na wakazi wakitazama kwa huzuni.
Kamanda wa Polisi wa Mwea Mashariki, Stephen Okal, alisema dereva wa lori alikuwa akielekea Embu kutoka Ngurubani alipojaribu kukwepa shimo na kuingia njia ya magari yaliyokuwa yakitoka upande wa pili, kabla ya kugongana na tuk-tuk hiyo.
Watu watano walifariki papo hapo, wawili wakafariki hospitalini baada ya kupelekwa Hospitali ya Kimbimbi Level Four. Lori hilo pia liligonga watembea kwa miguu wawili waliokufa papo hapo. Dereva wa tuk-tuk alikuwa miongoni mwa walioaga dunia.
Dereva wa lori, ambaye alipata majeraha madogo, alikamatwa na atafikishwa mahakamani baada ya uchunguzi kukamilika.
Miili ya marehemu ilipelekwa katika hifadhi ya maiti ya Hospitali ya Kerugoya Level Five huku magari yaliyoharibika yakipelekwa Kituo cha Polisi cha Wang’uru.
Mapema usiku wa kuamkia Jumamosi, mwanamke mmoja alifariki na watu wengine wanne kujeruhiwa vibaya katika ajali iliyohusisha magari kadhaa eneo la Mlima Nugu kwenye barabara ya Narok-Mai Mahiu.
Polisi walisema lori lililokuwa likielekea Narok lilipoteza mwelekeo na kuanguka mtaroni. Basi lililokuwa nyuma yake likaligonga kabla ya kugongana na gari aina ya Toyota Probox lililokuwa likitoka upande wa pili.
Majeruhi walikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Narok huku uchunguzi ukiendelea.
Ajali hizo zimetokea saa chache baada ya watu wengine 12 kufariki katika ajali mbili tofauti Alhamisi usiku.
Katika eneo maarufu la Mlima Punda kwenye barabara ya Eldoret-Nakuru, watu saba, akiwemo wanafunzi wawili waliokuwa wakirejea nyumbani kwa likizo, walifariki baada ya lori lililokuwa likipita magari mengine kugongana na matatu mbili.
Kamanda wa Polisi wa Uasin Gishu Wilberforce Sicharani alisema dereva wa lori alipoteza udhibiti alipokuwa akiteremka mlima na kugonga matatu zilizokuwa zikielekea Nakuru.
Kaunti ya Marsabit pia ilirekodi vifo vya watu watano baada ya trela moja kugonga nyingine katika Kargi Junction kwenye barabara ya Isiolo-Moyale. Wanne walifariki papo hapo huku mmoja akifariki hospitalini.
Visa hivyo vinafuatia ajali nyingine ya basi la shule katika Kaunti ya Meru wiki hii ambapo wanafunzi wawili walifariki na wengine 49, pamoja na walimu wanne na dereva, kujeruhiwa walipokuwa wakirejea kutoka ziara ya masomo.