Siasa

Ngome ya Raila yavuna vinono kwa kushirikiana na serikali

June 4th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

USHIRIKIANO kati ya Rais William Ruto na Kinara wa ODM Raila Odinga umefungulia eneo la Nyanza mifereji ya ustawi huku serikali ikiendelea na miradi ya maendeleo ambayo thamani yao ni Sh69 bilioni.

Kwa miaka mingi siasa za upinzani zimetenga eneo hilo kimaendeleo kwenye tawala zilizopita lakini kwa huu wa Kenya Kwanza, Nyanza inaendelea kutafuna vinono.

Tangu Bw Odinga na Rais Ruto wabuni Serikali Jumuishi mnamo Juni mwaka jana baada ya maandamano ya Gen Z, miradi mbalimbali imeanzisha Nyanza, eneo ambalo kiongozi wa nchi analenga kura zake mnamo 2027.

Katika Kaunti ya Kisumu, ngome ya siasa za Nyanza, mji unaendelea kungáa huku ujenzi wa miradi ukiendelea viungani mwa jiji, wanakandarasi wakijizatiti kukamilisha miradi kwa muda uliowekwa.

Ujenzi unaendelea wa barabara ya Chanan Sigh-Miwani kwa kima cha Sh14 bilioni pamoja na ile jirani ya Mamboleo hadi Chuo Kikuu cha Great Lakes kwa Sh9 bilioni.

Barabara hizo mbili zinatarajiwa kufungua zaidi jiji hilo linalokua kwa kasi zaidi likijizatiti kuwa kituo kikuu cha kibiashara ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Wiki jana, Rais alikuwa jiji hilo kufungua mradi wa ujenzi wa nyumba za gharama nafuu ambazo zitakuwa 15,000 kwenye awamu ya kwanza.

Rais alitangaza kuwa Bw Odinga ametoa ekari tano za ardhi ya familia yake eneo la Kirembe kwa serikali ya kitaifa kujenga nyumba hizo.

“Namshukuru Raila kutokana na wema wake na serikali itawekeza Sh3.5 bilioni kujenga nyumba kwenye ardhi hiyo ili kuwanufaisha karibu watu 1000,” akasema Rais Ruto.

Bw Odinga ambaye alikuwa naye aliahidi kushirikiana na Rais kuhakikisha suluhu inapatikana kwa changamoto za wananchi.

“Kila eneo linahitaji maendeleo na hatuwezi kuvumilia siasa za kikabila. Ujenzi wa nyumba hizi zitawasaidia wakazi wa Kisumu, shule zitajengwa na hospitali za kuwafaa raia pia zitakwepo,” akasema Bw Odinga.

Mpango wa kuhakikisha majitaka si kero Kisumu nao unaendelea kutekelezwa ambapo Sh1.2 bilioni zinatumika kujenga mradi wa mabomba ya kupitisha majitaka ya LVWATSAN kwa Sh1.2 bilioni.

Ujenzi wa Chuo Kikuu cha Tom Mboya unaelekea kukamilika kwa kima cha Sh1.23 bilioni na jengo la chuo hicho litawasitiri zaidi ya wanafunzi 10,000.

Taasisi ya Mafunzo Kuhusu Uvuvi na Uchumi wa Bahari/ Ziwa nayo ujenzi wake umekuwa ukiendelea wadi ya Kabonyo Kanyagwal, eneobunge la Nyando. Taasisi hiyo ambayo itakuwa ya kwanza nchini itawapa vijana mafunzo kuhusu ufugaji wa samaki na uvuvi na itakapokamilika, Sh2.5 bilioni zitakuwa zimetumika

Katika Kaunti ya Siaya, nyumbani kwa Raila, serikali imeanza ujenzi wa nyumba 882 ambazo zitagharimu Sh2.5 bilioni katika eneobunge la Alego Usonga.

Miradi mingine Siaya ni ujenzi wa barabara za Bondo-Uyawi-Liunda, Got-Nanga-Jera Bat Ober na Ukwala-Ugunja-Rwambwa kwa kima cha Sh4 bilioni.

Pia ujenzi unaendelea wa madaraja ya Dho-Gove na Nzoia ambapo Sh460 milioni zitatumika. Miradi ya maji ya Ugunja, Sega, Ukwala nayo ambapo Sh1.04 bilioni zilitumika, imekamilishwa na inawahudumia zaidi ya watu 91,000.

Masoko hayajaachwa nyuma huku yale ya kisasa yaliyojengwa Obamba, Akala, Sio Port, Riat Kolemo na Bar Ober kwa kima cha Sh300 milioni yakikamilika.

Kituo kikubwa cha kibiashara na viwanda nacho kinajengwa mjini Siaya na kitagharimu Sh500 milioni.

Katika Kaunti ya Homa Bay, miradi iliyoanzishwa na serikali kuu inaendelea kungárisha gatuzi hilo pamoja na mingine ya Gavana Gladys Wanga.

Serikali tayari imetumia Sh227 milioni katika ujenzi wa nyumba huku miradi mingine ikiwa ni ile ya maji Kendu Bay (Sh674 milioni), ya maji Oyugis (Sh1.37 bilioni) kisha barabara ya Mbita-Sindo-Kiabuya-Karungu-Agolo Muoko (Sh2.9 bilioni). Serikali pia imetumia Sh537 milioni kujenga masoko ya kisasa Homa Bay ambayo mengi yamekamilishwa.

Minofu ya Rais Ruto haijaacha Migori nyuma huku kazi ikiendelea katika barabara za Kadel-Ramba (Sh3.7 bilioni), Isebania-Ikerege-Kehancha-Ntimaru-Gitwembe-Angata (Sh2.86 bilioni) na Riosiri-Chuo Kikuu cha Moi (Sh1.18 bilioni), Masara-Sori (Sh1.52 bilioni)

Miradi mingine ni nyumba ya gharama nafuu, Mabera (Sh182 milioni) na umeme Migori (Sh277 milioni). Pia mradi ujenzi wa Kiwanda cha kawi cha Gogo umefufuliwa kwa kima cha Sh2.8 bilioni.

Kwa wakulima, mradi wa unyunyuziaji mashamba maji wa Lower Kuja umekamilika kwa asilimia 67 na utawasaidia kilimo kwenye ekari 1,000 za ardhi. Mradi huo umegharimu Sh89 milioni.

“Sisi tutaendelea kumuunga mkono Rais Ruto kwa sababu amekuja Migori mara tano tangu 2022. Uhuru Kenyatta (rais mstaafu) alikuja mara moja pekee kwa miaka 10 naye Mwai Kibaki (rais kati ya 2002-2013) alikuja mara moja na kupanda miti Sony,” akasema Mbunge wa Uriri Mark Nyamita.

Alisema ni katika utawala huu ambapo kaunti hiyo inajengewa uwanja wa ndege.

Isitoshe serikali imetumia zaidi ya Sh730 milioni kujenga masoko ya hadhi katika miji ya Riosiri, Ranen, Sibuoche na Ntimaru