Siasa

Ndoa kati ya Ruto na Oburu ni ya kulazimisha- TIFA

Na MWANDISHI WETU July 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

Wakenya wengi wanapinga ushirikiano wa kisiasa kati ya ODM na UDA, hali inayozua maswali kuhusu mustakabali wa mpango huo kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Haya ni kwa mujibu wa utafiti mpya wa kampuni ya Trends and Insights for Africa (TIFA) uliofanywa kati ya Juni 13 na 22, 2026, ukihusisha watu 2,048 kutoka kaunti zote 47 nchini na ambao matokeo yake yalitolewa Ijumaa.
Utafiti huo unaonyesha kuwa asilimia 52 ya Wakenya wanapinga Serikali Jumuishi, huku asilimia 30 pekee wakiunga mkono mpango huo. Asilimia 15 hawakuwa na maoni huku asilimia nne wakisema hawaufahamu ushirikiano huo.
Matokeo hayo yanaonyesha kuwa licha ya ushirikiano wa karibu miaka miwili kati ya Rais William Ruto na ODM kufuatia maandamano ya Gen Z ya mwaka 2024, bado umma haujaukubalika kwa kiwango kikubwa.
Kwa mujibu wa TIFA, kiwango cha uungwaji mkono kwa ndoa ya vyama hivyo kimeendelea kubaki karibu kilekile kwa mwaka mmoja uliopita. Kilikuwa asilimia 22 Mei 2025, kikaongezeka hadi asilimia 44 Agosti mwaka huo kabla ya kushuka hadi asilimia 30 Novemba 2025. Katika utafiti wa sasa, kimeendelea kusalia asilimia 30.
Ripoti hiyo inasema mgawanyiko unaoendelea ndani ya ODM kuhusu iwapo chama hicho kinafaa kuunga mkono azma ya Rais Ruto ya kutetea urais mwaka 2027 umefunga kiwango ambacho ushirikiano huo unaweza kupata uungwaji mkono.
Hakuna eneo lolote kati ya kanda tisa za utafiti lililoonyesha wengi wanaounga mkono ushirikiano huo.
Eneo la kati la Bonde la Ufa linaongoza kwa asilimia 47 ya wanaounga ushirikiano huo, likifuatiwa na Kaskazini mwa Kenya kwa asilimia 43 na Nyanza kwa asilimia 35. Magharibi ina asilimia 29, Pwani asilimia 31, Kusini mwa Rift Valley asilimia 25, Nairobi asilimia 22, Kusini Mashariki asilimia 30 na Mlima Kenya asilimia 13.
TIFA pia imebaini kuwa uungwaji mkono umeshuka kwa kasi zaidi Magharibi mwa Kenya, kutoka asilimia 62 Novemba 2025 hadi asilimia 29 sasa. Nyanza pia imeshuka kutoka asilimia 59 hadi 35, huku Mlima Kenya na Kaskazini mwa Kenya zikisajili kupungua kwa uungwaji mkono.
Ripoti hiyo inahusisha hali hiyo na mvutano unaoendelea ndani ya ODM kati ya makundi ya Linda Mwananchi na Linda Ground kuhusu mustakabali wa chama na ushirikiano wake na Kenya Kwanza. Viongozi kama Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi wameendelea kupinga ushirikiano wa karibu na serikali.
Wapigakura ambao hawajaamua Wakati huo huo, utafiti huo unaonyesha kuwa uchaguzi wa urais wa 2027 huenda ukaamuliwa katika maeneo yenye wapigakura wengi ambao bado hawajaamua upande wa kuunga mkono.
Mlima Kenya, wenye takriban wapiga kura milioni 5.7, umejitokeza kuwa uwanja mkubwa wa kisiasa. Asilimia 25 ya wakazi wa eneo hilo bado hawajaamua mgombea watakayemuunga mkono.
Nairobi pia imejitokeza kuwa uwanja muhimu wa kisiasa. Kalonzo anaongoza kwa asilimia 23, akifuatiwa kwa karibu na Sifuna kwa asilimia 22 na Matiang’i kwa asilimia 17. Rais Ruto anaungwa mkono na asilimia sita huku Gachagua akiwa na asilimia nane. Asilimia 21 ya wakazi wa jiji bado hawajaamua.
Pwani pia imeonekana kuwa eneo la ushindani mkali. Sifuna anaongoza kwa asilimia 27, Rais Ruto asilimia 21, Kalonzo asilimia 10 na Matiang’i asilimia tisa. Asilimia 21 ya wakazi bado hawajafanya uamuzi.
Katika eneo la Kusini Mashariki, Kalonzo ameendelea kutawala ngome yake kwa asilimia 58 dhidi ya asilimia 15 za Rais Ruto. Ni asilimia tisa pekee ambao hawajaamua.
Magharibi mwa Kenya pia inaonekana kuwa eneo litakaloamua matokeo ya uchaguzi. Sifuna anaongoza kwa asilimia 28, Rais Ruto asilimia 14 na Matiang’i asilimia 12. Hata hivyo, asilimia 31 ya wakazi bado hawajafanya uamuzi.
Kwa upande mwingine, Rais Ruto anaendelea kutawala Kaskazini mwa Kenya kwa asilimia 61 ya uungwaji mkono na bado ana nguvu katika baadhi ya maeneo ya Bonde la Ufa. Nyanza nayo inaendelea kuwa ngome ya upinzani, ingawa ushindani unaongezeka huku Matiang’i akipata asilimia 29 na Rais Ruto asilimia 30.
Kwa mujibu wa Katiba, mgombea wa urais lazima apate zaidi ya asilimia 50 ya kura halali pamoja na angalau asilimia 25 ya kura katika zaidi ya nusu ya kaunti zote nchini.
Kutokana na hali hiyo, TIFA inaeleza kuwa ushindi wa mwaka 2027 hautategemea tu ngome za kisiasa bali pia uwezo wa vyama kuwashawishi mamilioni ya wapiga kura ambao bado hawajaamua katika maeneo kama Mlima Kenya, Nairobi, Magharibi na Pwani.
Utafiti huo unatarajiwa kuathiri mikakati ya kampeni za kisiasa, huku Kenya Kwanza na viongozi wa upinzani wakiongeza juhudi za kuvutia wapigakura katika maeneo hayo muhimu kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.