Habari

TIFA: Sifuna sasa kifua mbele kupambana na Ruto 2027

Na RUSHDIE OUDIA July 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TAKRIBAN thuluthi mbili ya wafuasi wa kiongozi wa Democracy for the Citizens (DCP) Rigathi Gachagua wanaompinga Rais William Ruto wanaamini hafai kuwania urais mwaka ujao, bali amuunge mkono mgombeaji mwingine wa upinzani.

Haya ni kwa mujibu wa utafiti wa pili wa kitaifa wa kampuni ya Trends and Insights for Africa (TIFA) mwaka 2026, uliofanywa kati ya Juni 13 na 22 na kutolewa Ijumaa.

Utafiti huo pia unaonyesha kuwa Rais Ruto bado ndiye mgombeaji anayeungwa mkono zaidi kuwania urais huku uchaguzi mkuu ukisalia chini ya mwaka mmoja.

TIFA ilitoa chaguo tatu kuhusu nafasi ya Gachagua katika juhudi zake za kumng’oa Rais Ruto madarakani.

Miongoni mwa Wakenya wanaopinga kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto, asilimia 62 walisema Gachagua anafaa kumuunga mkono mgombeaji mwenye nafasi kubwa zaidi ya kushinda kutoka upinzani.

Ni asilimia 14 pekee waliotaka awe mgombeaji wa urais wa upinzani iwapo mahakama itamruhusu kugombea.

Iwapo mahakama itazuia kugombea, asilimia 29 ya Wakenya wanaamini anafaa kumuunga mkono mgombeaji mwingine wa upinzani. Hata kama ataruhusiwa kugombea, asilimia 33 bado wanaamini anafaa kumuunga mkono mgombeaji mwingine.

Asilimia tano pekee wanaamini Rais Ruto hawezi kushindwa bila kujali hatua ambayo Gachagua atachukua, huku asilimia 19 wakisema hawana uhakika.

“Matokeo yanaonyesha kuwa wapigakura wanaompinga Rais Ruto wanajali zaidi kuongeza nafasi za upinzani kushinda uchaguzi kuliko kujali nani atakuwa mgombeaji wake,” ilisema sehemu ya ripoti ya TIFA.

Kwa mujibu wa utafiti huo, Rais Ruto anaongoza kwa asilimia 24 ya uungwaji mkono.

Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna anafuatia kwa asilimia 15, aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i asilimia 14, kiongozi wa Wiper Patriotic Front Kalonzo Musyoka asilimia 13, Gachagua asilimia saba na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino asilimia mbili.

TIFA ilisema ingawa Rais Ruto bado ndiye mgombeaji anayependekezwa zaidi, kiwango chake cha asilimia 24 kinaonyesha upinzani bado una nafasi ya kushindana iwapo utaungana.

“Ingawa uungwaji mkono wa upinzani bado umegawanyika, Sifuna ameonyesha ongezeko kubwa zaidi la umaarufu. Umeongezeka kutoka kiwango kisichoweza kupimika mwaka 2025 hadi asilimia 15 mwezi Juni 2026, jambo lililomweka miongoni mwa wagombeaji wakuu wa upinzani,” ilisema ripoti hiyo.

Ndani ya ODM, Sifuna pia anaungwa mkono na asilimia 44 ya wanachama kama mgombeaji wa urais wa chama, ikilinganishwa na asilimia 20 wanaomuunga mkono Rais Ruto.

Kwa upande mwingine, umaarufu wa baadhi ya wanasiasa umeshuka.

Matiang’i alishuka kutoka asilimia 32 mwezi Mei 2025 hadi asilimia 14 mwezi Juni 2026.

Umaarufu wa Kalonzo nao umeshuka kutoka asilimia 25 mwezi Novemba 2025 hadi asilimia 13.

Kwa upande wa Sifuna, kiwango chake cha uungwaji mkono kimeongezeka kwa asilimia 50 tangu Mei, kutoka asilimia 10 hadi asilimia 15.

Umaarufu wa Babu Owino umeshuka kutoka asilimia nane mwezi Novemba mwaka jana hadi asilimia mbili, hali ambayo TIFA inaamini imetokana na baadhi ya wafuasi wake kuhamia kwa Sifuna.

Uungwaji mkono wa Gachagua pia umepungua kidogo, jambo ambalo TIFA inalihusisha na kushindwa kwake katika Mahakama Kuu kupinga kuondolewa kwake kama Naibu Rais.

Utafiti huo pia unaonyesha kuwa wanachama wa ODM wanaendelea kuunga mkono zaidi msimamo wa Linda Mwananchi huku ule wa Linda Ground ukiendelea kupoteza nguvu.

Kwa upande wa vyama vya siasa, ODM imeongeza uungwaji mkono kutoka asilimia 16 hadi 20, huku UDA ikisalia kwa asilimia 17.

Hata hivyo, DCP, Wiper, DAP-Kenya na Ford Kenya vimepungua kwa uungwaji mkono.

Kwa ujumla, TIFA ilisema ODM na UDA zimepoteza umaarufu tangu uchaguzi wa mwaka 2022, huku DCP ikiibuka kama mshindani mpya na karibu thuluthi moja ya wapigakura bado hawajaamua chama watakachounga mkono.

Kuhusu Serikali Jumuishi ya UDA na ODM, asilimia 52 ya Wakenya walisema wanaipinga, huku asilimia 30 wakisema wanaiunga mkono.

Asilimia 15 hawakuwa na maoni, huku asilimia nne wakisema hawajui kuhusu ushirikiano huo.

Kwa mujibu wa TIFA, kiwango cha uungwaji mkono kwa Serikali Jumuishi kimesalia karibu asilimia 30 tangu Mei mwaka huu.

Ripoti hiyo inaeleza kuwa ODM italazimika kuamua ikiwa ushirikiano huo ulikuwa wa muda mfupi wa kutekeleza ajenda ya mageuzi au utageuka kuwa ushirikiano wa muda mrefu.