Habari

Karua: Serikali za Kenya, Uganda zilishirikiana na Tanzania katika kudhulumu wanaharakati

Na KEVIN CHERUIYOT June 4th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

KIONGOZI wa chama cha People’s Liberation Party (PLP) Martha Karua amedai kuwa, serikali ya Kenya ilishirikiana na Tanzania kufanikisha kuzuiliwa na kufurushwa kwake kutoka taifa hilo jirani, licha ya kwamba yeye ni waziri wa zamani na wakili mkuu.

Katika kile kinachoonekana kama shutuma dhidi ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Bi Karua alielezea hofu kuhusu uwepo wa njama ya kunyamazisha viongozi wa upinzani katika ukanda huu.

Akielezea ukatili na kuzuiliwa kwa viongozi wa upinzani katika nchi za Uganda, Tanzania na Kenya, Bi Karua alitoa wito kwa raia kutetea haki zao na uhuru unaolindwa kwenye katiba.

“Tuungane na kupinga tawala dhalimu. Nataka kutangaza kuwa nchi tatu za Afrika Mashariki, Kenya, Uganda na Tanzania ni dhalimu na ningependa kuongeza kuwa Kenya ilishirikiana kufanikisha kuzuiliwa na kufurushwa kwangu na wazalendo wengine,” akasema Bi Karua.

Akihutubia wanahabari katika makao makuu ya PLP, Bi Karua alisema serikali ya Kenya ilisalia kimya huku raia wake wakizuiliwa, kudhulumiwa na kufurushwa kutoka Tanzania.

Hii, kulingana naye, ni licha ya kuwa, Rais William Ruto ni mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

Bi Karua alimkosoa Rais Ruto kwa kuomba msamaha kwa Tanzania na Uganda hata baada ya mwanaharakati Boniface Mwangi na wakili raia wa Uganda Agather Atuhaire kukamatwa na kudhulumiwa kinyume cha sheria.

“Dhuluma inapotumika, ni lazima kulikuwa na mawasiliano fulani. Walishirikiana. Hii ndiyo maana Kenya na Uganda ziliandika barua dhaifu siku moja. Barua ambazo hazikuwa na ukali wowote; hata zilichelea kuagiza kuwa balozi wa Tanzania aagizwe kuelezea walikozuiliwa Mwangi na Agather,” Bi Karua akaeleza.

Alisema kuna uwezekano Rais Ruto alijulishwa kuhusu dhuluma na mateso hayo.