Ghadhabu zaenea kuhusu mauaji ya Albert Ojwang licha ya polisi kituoni kutimuliwa
INSPEKTA Jenerali wa Polisi Douglas Kanja Jumatatu alithibitisha kuwa afisa wa ngazi ya juu kwenye idara ya polisi ndiye alikuwa mlalamishi kwenye kesi ambapo mwalimu na bloga Albert Ojwang alikamatwa.
Bw Kanja alidai kuwa mmoja wa manaibu wake ndiye alikuwa mlalamishi. Kukiri kwake sasa kulimweka Naibu Inspekte Jenerali wa Polisi Eliud Lagat kama mlalamishi.
“Kuna malalamishi ambayo yaliwasilishwa na afisi naibu inspekta jenerali wa polisi,” akasema Bw Kanja.
Bw Ojwang’ alikamatwa na akafa akizuiliwa na polisi kwa kuchapisha habari za uongo. Kifo chake kwenye seli za kituo cha polisi cha Central kimeibua ghadhabu za umma.
Jumapili jioni, Idara ya Polisi ilitoa taarifa zilizosema kuwa Afisa Msimamizi wa Kituo cha Polisi cha Central (OCS), polisi wa zamu, aliyesimamia seli na polisi wote waliokuwa kwenye kitengo cha kupokea malalamishi usiku huo, wametimuliwa kazini.
“Kuhakikisha kuwa uchunguzi huru unaendeshwa na Mamlaka Huru ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA), Inspekta Jenerali ameamrisha kutimuliwa kazini kwa maafisa hao,” ikasema taarifa hiyo iliyotiwa saini na Msemaji wa Polisi Michael Muchiri.
Umma jana uliendelea kuonyesha ghadhabu kutokana na mauaji ya Bw Ojwang’ huku wakiandamana hadi kituo cha Central. Bw Ojwang’ alikuwa amekamatwa nyumbani kwao Homa Bay kisha akaendeshwa kwa gari hadi Central.
Polisi awali walikuwa wamesema marehemu alipatikana akiwa amepoteza fahamu ndani ya seli baada ya kugongwa kichwa chake kwenye ukuta wa seli. Walidai alikufa alipokuwa akipelekwa Hospitali ya Mbagathi kwa matibabu.
Babake Ojwang, Bw Meshack Opiyo akibubujikwa na machozi alisimulia jinsi mwanawe alivyochukuliwa nyumbani kabla ya kula chakula cha mchana mnamo Jumamosi.
Alipelekwa hadi Kituo cha Polisi cha Mawego kabla ya kusafirishwa hadi Nairobi ambako alikufa mikononi mwa polisi.
“Polisi waliomkamata waliniambia Albert alikuwa amemkashifu mtu wa ngazi ya juu kupitia mtandao wa X,” akasema Bw Opiyo.
Bila kuwa na subira, babake naye aliabiri gari la umma na kuwafuata hadi Nairobi. Alipowasili katika kituo cha Central alifahamishwa kuwa mwanawe aliaga hospitalini.
Marehemu, mwalimu aliyekuwa akifundisha Voi alikuwa mtoto wa pekee kwa wazazi wake ambao wamekonga. Ameiacha familia changa akiwa na mtoto mwenye umri wa mwaka moja na mjane.
Kwenye sauti iliyonakiliwa, Bw Ojwang’ alisimulia masaibu yake kwa rafikiye Nairobi kuhusu kilichotokea. Kwenye sauti hiyo, rafiki huyo aliahidi kumtembelea Jumapili na wakakubaliana.
Bw Ojwang’ kwenye sauti hiyo iliyonakiliwa, alikuwa mchangamfu lakini alikuwa na wasiwasi wa kulala seli usiku huo.