Maoni

MAONI: ‘Macuzo’ watamtatiza Ruto

Na PAUL NABISWA June 10th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

NILIKUWA kati ya watu waliodhania kuwa aliyekuwa naibu Rais Rigathi Gachagua angezama kabisa kisiasa baada ya kufukuzwa kazi mwaka uliopita.

Bunge la taifa lilidhania kuwa ana tabia ovyo zisizoafiki taasisi ya Urais.

Bunge la seneti angalau likampa alama chache japo ratili ya tuhuma zilizokuwa zikimkabili ikawa nzito.

Mtoto wa Maumau jinsi anavyopenda kujiita akaambiwa kanyaga kubwa kubwa kama wanavyosema vijana wa leo.

Akaondoka kwa masikitiko, uso wake ukaonyesha mtu aliyelemewa na mzigo mzito wa siasa.

Wachache waliosalia naye hususan kutoka kati ya nchi wakatengwa na wenzao kama jini. Kumbe hawakumfahamu vizuri. Nami pia nilikuwa Tomaso.

Pamoja na kuwa baadhi ya watu kudhani kuwa alikuwa na ushamba fulani wa Mathira, ameonyesha sivyo. Kati ya wanasiasa wote wa upinzani amekuwa dhahiri zaidi na imara katika kuishambulia serikali ya Kenya kwanza kutumia mbinu bunifu.

Juzi akiwa ukambani akasema yeye ni “cousin” (binamu) ya Kalonzo Musyoka. Akaenda pwani ya Kenya na kufikisha tena ujumbe huo. Hii ni hesabu kali.

Gachagua anajenga dhana kuwa Mlima Kenya na Ukambani ni watu wa sehemu moja.

Hawa “macuzo” wa ukambani ndio waliomsadia Kibaki kupata muhula wa pili kwa kumpigia kura zote Kalonzo Musyoka katika uchaguzi wa 2007.

Si wengi lakini kura zao huwekwa mahali pamoja.

Hao “macuzo” walimpigia Raila Odinga kura kwa wingi katika uchaguzi wa 2013 hadi uchaguzi wa 2022.

Ni watiifu kwa “cuzo” mkubwa wa Rigathi Gachagua ambaye amewaambia wakati wa kuingia ikulu kwa mmoja anayepinga Rais wa sasa William Ruto ni wakati huu.

Japo Gachagua alitoa hoja kwa njia ya mzaha, inaweza kujenga jeshi kubwa la mapinduzi ya fikra miongoni mwa wapiga kura na kuwe na mwelekeo wa kikabila katika uchaguzi mkuu ujao.

Kwa misingi hii inavyoonekana wanaotaka kujihusisha na mwelekeo huo jamii za kibantu ambazo ni nyingi tu Kenya.

Hii sera ya Gachagua anaweza kutembeza magharibi mwa Kenya na sehemu nyingi na kuharibu hewa ya Rais Ruto katika baadhi ya sehemu alikodhania kuwa ameshika mizizi ya kisiasa.

Na sasa inavyoonekana hawa macuzo wanajumuisha Matiang’i ambaye jamii ya wabagusi baadhi ya watu wanasema ni yeye tu, Eugene Wamalwa na George Natembaya.

Huyu Gachagua mwenyewe alisema juzi Kiambu kuwa UDA Gatundu “tunafinish kumalo”.

Lugha hii ni ya vijana na anapotumia Riggy G ina maana anataka kuteka jumuiya pana ya vijana.

Hawa vijana ndio wanasema wakati huu kwenye mitandao “macuzo hi”. Jambo ambalo bado haliko wazi ni ikiwa hawa wanaojiita “macuzo” wataenda “nalonalo” jinsi wanavyosema Gen-Z.

Paul Nabiswa ni mhariri, NTV