Kindiki aahidi kutenganisha Kalonzo na Gachagua
NAIBU Rais Kithure Kindiki ameapa kuwa atamtafuta kinara wa chama cha Wiper Bw Stephen Kalonzo Musyoka, na kumleta serikalini.
Profesa Kindiki alisema kinara wa Wiper amekuwa akipotoshwa na wanasiasa wengine wenye nia mbaya, na ambao sera zake na zao haziambatani. Akizungumza katika hafla ya kuchangia akina mama pesa za kuwainua kibiashara katika eneo la Mutomo, Kitui Kusini, Naibu Rais alimtaka Bw Musyoka kujihadhari na wanasiasa kama aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua akidai kazi yake kuu imekuwa kuzunguka nchini kuwapotosha Wakenya na kuwagawanya kwa misingi ya kikabila.
Bw Kindiki pia aliwarai wakazi wa eneo hilo kuunga mkono serikali ya Kenya Kwanza ili iendelee kutekeleza miradi ya maendeleo akitoa mfano wa barabara kadhaa zitakazojengwa na pia miradi mingine ikiwemo ujenzi wa masoko. ‘Tayari serikali imetenga pesa za kujenga hii barabara ya Mutomo hadi Mutha. Pia tutakamilisha barabara ya kutoka Kibwezi kuja Kitui ambayo imekwama katika eneo la Kwa Siku, Mwingi magharibi,’ aliongeza Naibu huyu wa Rais. Kuhusu bajeti iliyosomwa Alhamisi, Kindiki alisema kuwa serikali haikuongeza ushuru wowote kwa Wakenya, bali ilizingatia zaidi ulipaji wa ushuru kwa wanabiashara na matajiri wanaokwepa kodi.
Aidha, alisema serikali itaziba mianya yote ya ubadhirifu wa pesa kupitia ufisadi.
ili kuhakikisha kuwa pesa zitakazokusanywa zinawafaidi wakenya ipasavyo. ‘Leo ningependa kuwahakikishia kuwa tutaziba mianya yote ya wizi wa mali ya umma, ili kuhakikisha kuwa hakuna pesa za umma zinatumika vibaya na maafisa wa serikali. Jukumu letu kuu ni kuwafanyia wakenya wote maendeleo na kuboresha uchumi wa nchi, bila kupoteza hata ndururu ya pesa tunazopata,’ akaeleza Kindiki.