Habari za Kitaifa

Gachagua, makanisa wamtaka Lagat aache kung’ang’ania kiti

Na GEORGE MUNENE, CECIL ODONGO June 16th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua Jumapili alimtaka Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat abebe msalaba wake kuhusiana na mauaji ya mwalimu na bloga Albert Ojwang.

Bw Gachagua alisema Bw Lagat anastahili kuchunguzwa, akamatwe na ashtakiwe, akisema kuuawa kwa Bw Ojwang ni ukosefu wa utu kwa thamani ya maisha ya binadamu.

“Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi, Mkuu wa Idara ya Upelelezi Nchini (DCI) wote waliohusika na mauaji hayo wanastahili kushtakiwa,” akasema Bw Gachagua ambaye alilalamika kuwa vijana wengi wameuawa kinyama katika utawala huu na hakuna hatua zozote ambazo zimechukuliwa.

“Kilichofanyika kwa Ojwang ni kionjo kwa sababu vijana wengi wameteswa kisha kuuawa na kikosi spesheli cha polisi maarufu kama 101, utekaji nyara na mtindo wa mauaji nchini unashangaza sana,” akaongeza Bw Gachagua.

Naibu huyo wa rais aliyeondolewa mamlakani mnamo Oktoba mwaka jana, alisema serikali ndiyo inastahili kuwajibika kutokana na mauaji na utekaji nyara ambao umekuwa ukishuhudiwa nchini.

Alikuwa akiongea jana kwenye Kanisa la Holyspirit Kagio Kaunti ya Kirinyaga ambako aliandamana na viongozi wengine wa upinzani akiwemo Kiongozi wa PLP Martha Karua.

Huku Bw Gachagua akisukuma sana Bw Lagat ajiondoe, makanisa nayo hayajamwacha naibu huyo inspekta jenerali wa polisi apumue.

Jumapili, Muungano wa Makanisa Nchini (KCCAM) pia ulitoa wito kwa polisi wote ambao wamehusishwa au kutajwa kwenye mauaji ya Bw Ojwang’ wajiondoe madarakani.

“Tunatoa wito kwa uchunguzi ufanyike kuhusu mauaji ya Albert Ojwang pamoja na mauaji ya vijana wengine. Maafisa wote ambao walihusika kwa njia moja au nyingine akiwemo Lagat ambaye alitajwa alikuwa mlalamishi, wanastahili kuondoka kazini hadi uchunguzi ukamilike,” akasema Mwenyekiti wa KCCAM Askofu Kepha Omae.

Maaskofu hao pia walitoa wito kwa Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja aingilie kati na asiwaruhusu polisi watibue maandamano yanayotarajiwa kuendelezwa wiki hii na makundi mbalimbali kusaka haki kwa Bw Ojwang’

“Tunapowaomba maafisa wa polisi wasiwakabili waandamanaji, pia tunatoa wito watoe ulinzi na kuwakamata waporaji na wahalifu ambao wanatumia maandamano haya kuendeleza maovu yao,” akaongeza Bw Omae.

Kikao cha jana kilihudhuriwa na maaskofu 15 ambao wanatoka makanisa mbalimbali nchini.