Ruto anavyotumia mbinu zile zile za zamani kuhujumu Upinzani
UAMUZI Bodi inayosimamia viwanja nchini (Sports Kenya) kumnyima aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua uwanja wa kutumia kuendesha hafla ya uzinduzi wa chama chake kipya, tukio hilo limeamsha kumbukumbu kuhusu mbinu za zamani zilizotumiwa na serikali kuhujumu upinzani.
Chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP) kimelazimika kusaka mahala pengine pa kuandalia hafla hiyo baada ya kuzuiwa kutumia uwanja wa michezo wa kimataifa wa Kasarani, Nairobi, Juni 3, 2025.
Hata hivyo, hiyo ni mbinu ya zamani ambayo imetumika na serikali zilizopita kuwanyima viongozi wa upinzani nafasi ya kuandaa mikutano ya kisiasa.
Ilisemekana kuwa Bw Gachagua alinyimwa nafasi ya kuandaa hafla ya uzinduzi wa DCP baada ya taarifa za kijasusi kubaini kuwa huenda fujo zingetokea na shughuli za ukarabati zinazoendelea katika uwanja huo wa Kasarani. zingetatizika.
Aidha, maombi kama ya Bw Gachagua yamekuwa yalikataliwa kutokana na kukodiwa kwa uwanja wa Kasarani kwa shughuli nyingine.
Awali awali Sports Kenya ilikuwa imekubali ombi la Chama cha DCP kwamba kitumie uwanja wa Kasarani mnamo Juni 3, 2025. Usimamizi wa uwanja huo ulikitumia chama cha DCP taarifa ya malipo ya Sh3.7 milioni.
“Tunasikitika kukueleza kuwa hamtapata nafasi ya kutumia uwanja huo kwani ulikuwa umekodiwa kwa matumizi ya timu za michezo. Aidha, hatupokei maombi mengine ya matumizi ya uwanja huu kutokana na matayarisho ya michuano ya Kombe la Afrika kwa Wachezaji wa nyumbani (CHAN, 2025) itakayoandaliwa katika uwanja wa Kasarani,” Sports Kenya ikasema ikikataa ombi la DCP.
Kiongozi wa ODM Raila Odinga amedhulumiwa mara kadhaa na serikali kwa kunyimwa nafasi ya kuandaa mikutano ya chama chake katika viwanja vya umma.
Wakati wa utawala wa Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta maafisa wa polisi walifutulia mbali mikutano yake kwa kisingizio kuwa ingekumbwa na fujo.
Wakati fulani, serikali ya Jubilee ilikodi viwanja vyote vikuu, kuelekea uchaguzi mkuu wa 2017, ili kumzuia Odinga, wakati huo akiwa kiongozi wa muungano wa upinzani, NASA, kuandaa mikutano ya kampeni.
Wakati fulani, kinyesi cha binadamu kilimwagwa katika uwanja wa Jacaranda, eneo bunge la Embakasi Mashariki, Nairobi, kumzuia Bw Odinga na wafuasi wake kufanya mkutano hapo.
Rais Ruto pia alikumbwa na masaibu kama hayo baada ya kukosana na aliyekuwa bosi wake, Bw Kenyatta, hasa kuelekea uchaguzi mkuu wa Agosti 2022.
Bw Kenyatta pia alimeza dawa yake, pale ambapo baada ya kuondoka afisini, alinyimwa nafasi ya kuandaa Kongamano la Kitaifa la Wajumbe (NDC) la chama chake cha Jubilee katika ukumbi wa Bomas of Kenyatta.
Bw Kenyatta alilazimika kusaka uwanja mwingine wa kibinafsi kuendeshea shughuli hiyo.