Akili MaliMakala

Wabunifu wahimizwa kuunda teknolojia nafuu za kilimo

Na SAMMY WAWERU August 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WABUNIFU katika sekta ya kilimo na mabadiliko ya tabianchi wamehimizwa kuunda teknolojia za bei nafuu, rahisi kutumia na endelevu zinazolenga mahitaji halisi ya wakulima wa mashamba madogo, ambao huzalisha zaidi ya asilimia 75 ya chakula kinachotumiwa nchini Kenya.

Mkurugenzi Mkuu wa KickStart International, Peter Juma, anasema wakulima hawawezi kutumia teknolojia kwa sababu tu ni bunifu, bali huchagua suluhisho zinazoshughulikia changamoto zao, za bei nafuu na zinazowapa faida.

“Wakulima hutumia teknolojia ikiwa ni ya bei nafuu, inatatua tatizo halisi na inajilipa,” akasema Bw Juma.

Mjasiriamali huyo wa teknolojia za kilimo alikuwa akizungumza katika kongamano la Kenya Editors Guild (KEG) Press Club lililofanyika Nairobi, lililowaleta pamoja wanahabari na wahariri wa masuala ya kilimo, pamoja na washikadau wengine katika sekta hiyo.

Kongamano hilo “Resilient Harvests” na kaulimbiu “Building Climate-Smart Agriculture for Kenya’s Future”, liliwakutanisha watunga sera, wanasayansi, wabunifu, washirika wa maendeleo, wakulima na wanahabari kujadili njia za kujenga kilimo kinachoweza kustahimili athari za mabadiliko ya tabianchi.

Ingawa washikadau wanaendelea kuhimiza matumizi ya teknolojia za kidijitali na ubunifu katika kuimarisha mifumo ya chakula, Juma alisema wakulima wengi wanahitaji suluhisho rahisi kutumia, kutunza na kumudu kifedha.

Trekta ndogo ikilima shamba. Picha|Sammy Waweru

Alisema pia teknolojia za kilimo zinapaswa kuzingatia mahitaji ya jinsia, kuwa nyepesi na zinazoweza kubebwa ili ziweze kutumiwa na watu wengi zaidi.

“Teknolojia kama pampu za maji zinapaswa kutengenezwa ili zitumike katika mazingira tofauti, ikiwemo maji safi na yenye chumvi, na ziweze kuendana na maeneo mbalimbali nchini,” alisema.

Juma alibainisha kuwa teknolojia nyingi za kilimo, zikiwemo pampu za maji zinazotumia nishati ya jua na mashine za kilimo, bado ni ghali kwa wakulima wa mashamba madogo.

“Pampu ya maji inaweza kugharimu Sh40,000 pekee, huku aina nyingine ikiuzwa hadi Sh200,000, ilhali zote huuzwa kama suluhisho kwa wakulima wa mashamba madogo,” alisema.

Alisisitiza kuwa wabunifu wanapaswa kuzingatia uwezo wa kifedha wa wakulima wakati wa kubuni teknolojia.

“Wakati wa kuunda teknolojia, wanaozibuni lazima wazingatie bajeti na mahitaji ya wakulima ili tujenge uwezo wa kukabiliana na athari mbaya za mabadiliko ya tabianchi,” aliongeza.

Washiriki wa kongamano hilo walikubaliana kuwa Kenya haina uhaba wa suluhisho, tafiti au data kuhusu tabianchi. Changamoto kubwa ni kubadilisha maarifa hayo kuwa hatua zinazoweza kutekelezwa, kufikiwa na kupitishwa kwa urahisi na wakulima.

Mayai kwenye mtambo wa kisasa kuyaangua vifaranga. Picha|Sammy Waweru

Majadiliano yalilenga jinsi mabadiliko ya tabianchi yanavyobadilisha mifumo ya kilimo, yakiathiri mazao yanayopandwa, kiwango cha mavuno na hatimaye upatikanaji wa chakula katika familia za Kenya.

Washiriki walisema utafiti unaomlenga mkulima, ushirikiano bora wa taasisi, suluhisho zilizojaribiwa nchini na mawasiliano yanahitajika ili kusaidia wakulima kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Aidha, walisisitiza kuwa nafasi ya vyombo vya habari katika kuangazia suluhisho, uwajibikaji na uzoefu wa jamii zinazokabiliana na mabadiliko ya tabianchi, badala ya kuangazia majanga pekee.

“Wanahabari na wahariri si watazamaji tu wa mabadiliko ya tabianchi. Sisi ni wasimuliaji wanaoleta uzoefu wa binadamu kwa umma, walinzi wanaowawajibisha taasisi na wawezeshaji wanaosaidia kuunda uelewa kwa umma,” alisema Agnes Mwangangi, Mjumbe wa Baraza Kuu la Kenya Editors Guild.

Kongamano hilo pia lilibainisha fursa nyingi zilizopo katika kilimo cha Kenya, hasa katika teknolojia na ubunifu.