Habari

Ruto alivyojikaanga kuhusu ahadi ya kukomesha utekaji nyara, mauaji

Na KAMORE MAINA June 16th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

BAADA ya Rais William Ruto kuingia madarakani aliahidi kuwa angepambana na utekaji nyara na kuvunja kabisa vikosi vya siri vya polisi vilivyokuwa vikiendeleza mauaji.

Licha ya ahadi hiyo, hali haionekani kubadilika. Baada ya kuapishwa, Rais alivunja kikosi spesheli cha polisi ambacho kilishutumiwa kuyatekeleza mauaji ya kiholela.

Wakati akiwa naibu rais, kiongozi wa nchi alikuwa amevamiwa na wale walioaminika kuwa maafisa wa usalama wa serikali ya mtangulizi wake Rais Uhuru Kenyatta.

Alisema kuwa katika uongozi wake vitengo vya usalama vingefanya kazi kivyao tena kwa njia huru bila kuingiliwa na yeyote.

Wakati huo raia wawili kutoka India ambao walikuwa sehemu ya kamati ya kampeni yake walikuwa wametoweka na tukio hilo lilimkasirisha huku akiapa hangevumilia mauaji ya kiholela.

“Mauaji ya kiholela lazima yakome kwa sababu ni haramu, si ya kikatiba na yanakiuka haki ya kuishi,” akasema Rais Ruto kwenye Ikulu ya Nairobi wakati wa mkutano na wanachama wa Tume Huru ya Kutathmini Utendakazi wa Polisi (IPOA).

Wakati huo rais aliamrisha kikosi cha SSU ambacho kilihusishwa na kutokomea kwa raia hao wawili kutoka India Zulfiqar Ahmad Khan na Mohamed Zaidi Sami Kidwa, kivunjwe.

Aliagiza polisi ambao walihusishwa katika kutokomea kwa wawili hao na dereva wao wa teksi Nicodemus Mwania, washtakiwe kwa mauaji.

Kufuatia uchunguzi ulioendeshwa na wakati huo Mkuu wa Kitengo cha Masuala ya Ndani Kiuslama Mohamed Amin (sasa mkuu wa DCI), watu 15 walinyakwa akiwemo maafisa kutoka Kitengo cha Ujasusi (NIS) na Shirika la Huduma kwa Wanyamapori (KWS) walikamatwa.

Mnamo Juni 20, 2024 baada ya kumaliza miezi kadhaa korokoroni, Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Renson Ingonga aliidhinisha mashtaka ya mauaji dhidi ya polisi hao 15.

Walishtakiwa kwa utekaji nyara na kutoweka kwa raia hao wawili kutoka India na dereva wao wa teksi kati ya Julai 22 na Julai 23, 2022 Nairobi.

Hata hivyo, siku 1,000 baadaye, utawala huu bado unashutumiwa kwa mauaji ya kiholela na watu kupotea kwa njia tatanishi.

Wakati wa maandamano ya Gen Z mwaka jana, kulikuwa na utekaji nyara na kuteswa kwa vijana ambao walihusishwa na maandamano yaliyokuwa yakishuhudiwa.

Ripoti ya Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu ilionyesha watu 50 waliuawa, 59 walitekwa nyara na maafisa wa usalama huku 413 wakijeruhiwa na polisi.

Hadi leo hakuna afisa wa polisi ameshtakiwa kwa mauaji au kuhusu utekaji nyara wakati wa maandamano hayo. Kesi pekee ambayo inaendelea ni ile ya kupigwa risasi kwa Rex Maasai ambaye alikuwa akiandamana.

Wakati wa maandamano kitengo ambacho kinaongozwa na afisa wa zamani wa DCI na sasa anahudumu kwenye NIS alitwikwa jukumu la kuwakabili waandamanaji na wafadhili wao.

Waliokuwa wakikamatwa walizuiliwa kwa siku kadhaa jijini na kuteswa. Maafisa hao walitoka DCI, NIS na idara nyingine za kiusalama na baadhi hata walikuwa wakitumia teknolojia ya kisasa kuwakabili waandamanaji kutoka makao makuu ya DCI.

Mnamo Mei 12, Rais aliamrisha wote waliokuwa wakizuiliwa waachiliwe huru na waungane na familia zao huku akiahidi utekaji nyara haungefanyika tena.

Alikuwa akiongea baada ya kukutana na Rais wa Finland Alexander Stubb ikuluni.