Habari za Kitaifa

Ufichuzi: Silaha za Kenya zapatikana katika vita nchini Sudan

Na MIKE YAMBO, JACKLINE MACHARIA, CARLOS GONZALES June 16th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

“KUNA majenerali wawili wasiothamini maisha ya mwanadamu. Vita nchini Sudan vinaelekea kuwa janga la mauaji ya kibinadamu. Juhudi zifanyike katika ukanda huu, na ulimwenguni, kuzuia mauaji haya, mateso kwa wanadamu na janga linalonukia nchini Sudan.”

Haya yalikuwa maneno ya Rais William Ruto mnamo Mei 31, 2025 kwenye kikao na wanahabari katika Ikulu ya Nairobi.

Alisema hayo alipomkaribisha Rais wa Slovenia Nataša Pirc Musar, na kuorodhesha mapigano kadhaa katika mataifa jirani na jinsi Kenya imehusika katika kuleta upatanishi kati ya pande hasimu.

Vita vilipochacha nchini Sudan 2023, Kenya ilihusishwa katika juhudi za kuleta amani ambapo Rais Ruto aliteuliwa na Shirika la Maendeleo la IGAD kuwa Mpatanishi Mkuu.

Alikutana na Jenerali Abdel Fattah al-Burhan, Rais aliyeteuliwa na Baraza Kuu la Mpito, kufuatia mageuzi ya kijeshi yaliyotokea nchini humo mnamo 2019.

Dkt Ruto alifanya mkutano huo katika Ikulu ya Nairobi mnamo Novemba 2023.

Kisha mnamo Januari 2024 alikutaka na Mohamed Hamdan Dagalo, almaarufu Hemedti, aliyekuwa naibu mwenyekiti wa Baraza la Mpito Nchini Sudan ambaye pia ni mkuu wa mkuu wa kundi la waasi la Rapid Support Forces (RSF), jijini Nairobi.

Ulikuwa ni mkutano wa faragha na ulipomalizika Rais Ruto alisema alifurahishwa na “kujitolea kwa RSF na kiongozi wake (Hemedti) kusitisha vita nchini Sudan kupitia mazungumzo.

Mnamo Januari 2025, Amerika ilimwekea Hemedti vikwazo kwa kuendeleza mauaji ya halaiki, mauaji ya kikabila na kuzuia kuwasilishwa kwa misaada ya kibinadamu katika vita vya wenyewe kwa wenyewe vinavyoendelea nchini Sudan”.

Sasa uchunguzi wa miezi sita ulioendeshwa na Shirika la Habari la Nation (NMG) kwa ushirikiano na Bellingcat umefichua uwezekano wa Kenya kuhusika katika vita nchini Sudan.

Kuhusika kwa Kenya, sio katika juhudi kwa kukomesha vita hivyo bali ni kutoa usaidizi wa silahi kwa upande mmoja— RSF.

Katika video iliyowekwa kwenye mtandao wa X mnamo Mei 23, 2025, jeshi la ulinzi la Sudan (SAF) wapiganaji wanaoliunda mkono wanaonekana wakifanya msako katika depo moja iliyotelekezwa na wapiganaji wa RSF.

Ndani ya depo hiyo kuna mirundo ya kreti na masanduku kadhaa yaliyotengenezwa kwa mbao.

Wanajeshi wa Sudan wanasherehekea kunaswa kwa silaha hizo na katika ujumbe wao kwa RSF wanasema, “ungewezaje kutorokana kuacha nyuma silaha nyingi kiasi hiki.”

Ukitazama kwa makini unaona neno “Kenya” likiwa limeandikwa kwenye kreti na masanduku hayo.

Maswali muhimu yanaibuliwa. Video hizi zilinaswa wapi?

Ripoti za vyombo vya habari zinasema kuwa uvamizi ulifanywa na wanajeshi wa SAF katika eneo la Omdurmna, mjini wa pili kwa idadi kubwa ya watu, ulioni karibu na ufuo wa Mto Nile-umbali wa kilomita 10 kaskazini mwa Khartoum.

Kutolewa kwa ripoti hizo kunalandana na maeneo kwenye video hizo na wakati ambapo ziliwekwa mitandaoni.

Mnamo Mei 20, Jenerali Al-Burhan, mkuu wa jeshi la SAF, alitangaza kuwa jimbo la Khartoum lilikuwa huru kutoka udhibiti wa wapiganaji wa RSF.

Jimbo hilo linajumuisha mji wa Omdurman na ule wa Khartoum Kaskazini.

Tulichambua video hizo ili kupata maelezo yake. Haya yalikuwa miongoni mwa video vilivyowekwa kwenya akaunti za watetezi wa SAF ambazo zilikuwa zikitokea katika kitongoji kimoja cha mji wa Omdurman, ndani ya jimbo la Khartoum.

Video vinavyoonekana kunaswa ndani ya chumba kimoja, zinaonyesha kuwa kreti za silaha huenda zilihifadhiwa katika depo moja chini ya ardhi.

Maelezo hayo yanalandana na yale ya video iliyoandamanishwa na habari iliyopeperushwa na shirika la Habari la Russian Today Arabic, iliyoonyesha kuwa uvamizi huo uliendeshwa katika jengo lenye vyumba chini ya ardhi.

Justin Lynch, Mkurugenzi Mkuu wa shirika la kufuatilia mizozo, Conflict Insights Group na mtafiti nchini  Sudan, anasema kugunduliwa kwa kreti zenye silaha zenye kibandiko cha jina “Kenya” ni ithibati kwamba Kenya inaunga mkono RSF kisiasa na kisilaha.

-IMETAFSIRIWA NA CHARLES WASONGA