Hofu ya watoto kutoka familia maskini kuacha shule serikali ikipunguza bajeti ya chakula
MAELFU ya wanafunzi kutoka familia maskini wanakabiliwa na hatari ya kuacha masomo baada ya serikali kukata sehemu kubwa ya ufadhili wa mpango wa kuwapa wanafunzi chakula shuleni.
Mgao ambao umeelekezwa kwenye mpango huo umepungua kutoka Sh4.9 bilioni hadi Sh3 bilioni. Kiasi hicho ni chini ya kile ambacho kilipendekezwa na Wizara ya Elimu cha Sh7.2 bilioni.
Mpango wa kula shuleni huwasaidia zaidi ya wanafunzi milioni 2.65 kutoka familia maskini katika kaunti 26, wengi wao wakiwa wa kutoka maeneo kame.
Baada ya kupunguzwa kwa mgao huo wa chakula shuleni, kuna hofu watoto hawa huenda wakaacha masomo na kupunguza takwimu kuhusu idadi ya wanafunzi shuleni kote nchini.
Uamuzi wa kupunguza bajeti kwa karibu Sh2 bilioni unakinzana na ahadi aliyoitoa Rais William Ruto na viongozi wengine wa Serikali ya Kenya Kwanza wakati wa kampeni za kuelekea uchaguzi mkuu wa kura za mwaka wa 2022.
Katika manifesto yao, waliahidi kuongeza fedha mara mbili zaidi kwenye mpango wa kuwapa watoto chakula shuleni.
Walilenga pia kuongeza idadi ya wanafunzi wanaonufaika na mpango huo kutoka milioni mbili hadi milioni nne.
Pia uongozi wa Kenya Kwanza uliahidi kuongezea kaunti pesa ambazo si mkopo ili kupiga jeki mpango huo ndipo idadi ya wanaonufaika kutoka shule za chekechea hadi shule za msingi ipande na kufikia milioni nane.
Bajeti iliyosomwa wiki jana inakiuka ahadi hiyo na kurejesha nyuma hatua ambazo zilikuwa zimeanza kupigwa katika sekta ya elimu tangu Rais Ruto achukue mamlaka.
Wakati akitoa ahadi hiyo enzi za kufanya kampeni, mpango huo ulikuwa na bajeti ya Sh1.96 bilioni.
Kwa sasa mgao wa Sh3 bilioni japo upo juu kidogo, bado ni kiasi cha chini kuliko pesa ambazo Rais Ruto aliahidi kuongeza maradufu ambazo ni Sh3.92 bilioni.
Pia idadi ya wanafunzi wanaonufaika imepanda kwa kiasi kidogo kutoka 2,538,200 mnamo 2022 hadi 2651,600 mnamo 2025. Hii ni ongezeko la 113,330, idadi ya chini ya milioni nne ambayo ilikuwa inalengwa.
Kupunguzwa kwa bajeti ya mpango huo kunatokea wakati ambapo miradi mingine ya serikali imeongezewa hela.
Kwa mfano, mgao wa kukarabati Ikulu ya Nairobi na ikulu ndogo kote nchini, umeongezwa kwa Sh894.9 milioni na bajeti hiyo sasa imepanda hadi Sh2.3 bilioni.
Aidha, pesa ambao zimetengewa ukarabati wa Jumba la Harambee na Mchapishaji wa Serikali imeongezwa kutoka Sh50 milioni hadi Sh1.46 bilioni.
Pesa za kukarabati Ikulu na ikulu ndogo kuongezwa, kumechangia ghadhabu za umma, raia wakiuliza iwapo serikali inajali maslahi ya raia na haki ya kupata elimu.