Korti yawazima Wetang’ula, Kingi kushiriki kampeni za Ruto Tutam
SPIKA wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula na mwenzake wa Seneti Amason Kingi wanakabiliwa na kesi ya kikatiba inayoweza kubadili mipaka ya ushiriki wa viongozi wa Bunge katika siasa za uchaguzi.
Hii ni baada ya Mahakama Kuu kuwazuia kwa muda kushiriki kampeni za kumrejesha Rais William Ruto mamlakani mwaka wa 2027 kwa kutumia mamlaka ya nyadhifa zao.
Mahakama ilitoa amri za muda zinazowazuia wawili hao kutumia mamlaka, hadhi, ushawishi au heshima ya afisi zao za kikatiba kuandaa, kuendesha, kuunga mkono au kuendesha kampeni za kisiasa hadi kesi hiyo itakaposikizwa na kuamuliwa.
Kesi hiyo iliwasilishwa na shirika la kiraia la Vocal Africa, ambalo linasema kushiriki kwa maspika hao katika kampeni za kisiasa kunadhoofisha uhuru wa Bunge na kuvunja mpaka uliowekwa na Katiba kati ya Bunge na Serikali Kuu.
Mahakama ilitambua kesi hiyo kuwa ya dharura na kuagiza maspika hao kuwasilisha majibu yao ndani ya siku tatu za kazi.
Kesi hiyo itatajwa Julai 16 kwa maelekezo zaidi.
Mbali na Wetang’ula na Kingi, walioshtakiwa ni Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) pamoja na Mwanasheria Mkuu.
Katika kesi yake, Vocal Africa inasema Katiba iliunda Bunge kama mhimili huru unaopaswa kusimamia Serikali Kuu, na hivyo viongozi wake hawapaswi kuonekana kama viongozi wa kampeni za kisiasa.
“Katiba iliunda Bunge ambalo lingesimama bega kwa bega na Serikali Kuu, si kuwa nyuma yake. Iliwakabidhi maspika wa bunge mamlaka ya kikatiba, si kwa manufaa ya kisiasa ya chama; iliwapa jukumu la kulinda na kuongoza taasisi ya Bunge, si kuendesha kampeni za uchaguzi,” zinasema stakabadhi za kesi hiyo.
Shirika hilo linadai kuwa kati ya Juni na mapema Julai mwaka huu, Bw Wetang’ula alihudhuria mikutano ya kisiasa Likoni (Mombasa), Emuhaya (Kakamega) na Eldoret (Uasin Gishu), ambako alidaiwa kuhimiza wananchi kumuunga mkono Rais Ruto na ajenda za serikali ya Kenya Kwanza.
Naye Bw Kingi anatuhumiwa kushiriki mikutano ya uhamasishaji wa kisiasa Mombasa na maeneo mengine ya Pwani.
Kwa mujibu wa walalamishi, hatua hizo zimeibua mgongano kati ya wajibu wa maspika hao wa kuongoza Bunge kwa njia isiyoegemea upande wowote na shughuli zao za kisiasa, jambo ambalo limepunguza imani ya umma kwa uhuru wa Bunge.
“Mamlaka ya kikatiba ya Bunge hayawezi kutekelezwa ipasavyo ikiwa maafisa wa kikatiba waliokabidhiwa jukumu la kuongoza mabunge yote mawili watajitokeza hadharani kama viongozi wa kampeni za kisiasa au watetezi wa kuchaguliwa tena kwa Serikali ile ile ambayo Bunge lina wajibu wa kusimamia na kuwajibisha kwa mujibu wa Katiba,” walalamishi wanasema.
Vocal Africa inasema kwamba haipingi haki ya maspika hao kuwa na misimamo ya kisiasa binafsi, bali inapinga matumizi ya mamlaka na heshima ya afisi zao za kikatiba katika kampeni za uchaguzi.
Shirika hilo linaomba mahakama itoe amri ya kudumu ya kuwazuia kutumia nyadhifa zao kwa shughuli za kampeni, itangaze kuwa vitendo hivyo vinakiuka Katiba na misingi ya uongozi bora, uadilifu na imani ya umma, na pia iamuru IEBC pamoja na EACC kuchunguza madai hayo na kuwasilisha ripoti zao mahakamani.