Makala

Hofu ya washirika wa Ruto Mlima Kenya uasi ukienea

Na MWANGI MUIRURI June 18th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WASHIRIKA wa Rais William Ruto katika eneo la Mlima Kenya wameingiwa na hofu kubwa kufuatia uasi unaozidi kushika kasi dhidi ya serikali, hali inayowaweka katika hatari ya kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Wasiwasi wao mkubwa ni kwamba ikiwa Rais Ruto akiamini kuwa Mlima Kenya hautamuunga mkono kwa muhula wa pili, anaweza kutafuta mgombea mwenza kutoka eneo jingine.

Aidha, huenda akalazimika kubadilisha nia na kutotumia chama cha UDA ambacho ndicho kilichowawezesha wengi wao kuingia mamlakani mwaka 2022.

Tayari, Rais ameanza kumshawishi Mkuu wa Mawaziri, Musalia Mudavadi, kuunganisha chama chake cha ANC na UDA.

Kiongozi wa The Service Party, Mwangi Kiunjuri, aliambia Taifa Leo kwamba mipango ipo ya kuunda muungano na vyama kutoka Mlima Kenya kumsaidia Rais Ruto kwenye azma yake ya 2027.

“Vyama hivyo vitadhamini wagombeaji wanaomuunga mkono Rais Ruto. Chama changu ni mojawapo na kitapendekeza Ruto kuwa mgombea wa urais,” alisema Kiunjuri.

Aliongeza kuwa mpango upo wa kuwa na wawakilishi katika kaunti kutoka vyama vinavyounga Ruto kusaidia kuchochea ushawishi mashinani.

Pia alihimiza viongozi wote waliochaguliwa Mlima Kenya waanze kuimarisha vyama vyao mapema.

Mwakilishi wa Wanawake Murang’a, Bi Betty Maina, alionya kuwa uhasama dhidi ya Rais unaweza kuathiri maendeleo katika eneo hilo hadi mwaka 2032.

“Urais ni kama ng’ombe wa maziwa. Hauwezi kuikama huku ukiipigia kelele. Serikali huenda pale inapopendwa,” alisema.

Hali imechacha zaidi baada ya aliyekuwa Naibu Rais, Rigathi Gachagua, kuzindua chama kipya cha Democracy for Citizens Party (DCP) ambacho anasema ni chombo maalum cha kisiasa kwa Mlima Kenya kuelekea 2027.

“DCP ina ajenda mbili kuu: Kumuondoa Rais Ruto madarakani kupitia kura ya 2027 na pia kuwaondoa wafuasi wake wote kutoka uongozi,” alisema Gachagua.

Lakini Kiunjuri amepinga vikali kauli hiyo na kuitaja kama ndoto ya mchana:

“Tutaangalia kama kura za Mlima Kenya zitagawanyika kwa nusu ama nyingi ziende kwa Rais Ruto,” alisema.

Gachagua alidai kuwa kampeni zake zimeleta hofu ndani ya kambi ya Rais na kwamba kuna juhudi za Rais kuunda chama kipya kwa kushirikiana na vyama vya vidogo kutoka Mlima Kenya.

Kulingana na Bw Jamleck Kamau, mshirika wa zamani wa Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, hali ndani ya kambi ya Rais Ruto ni ya hofu na taharuki.

“Tulijifunza kwa uchungu kuwa pesa, vitisho au taasisi za serikali haziwezi kushinda matakwa ya wananchi,” alisema Kamau, ambaye sasa amejiunga na DCP.

Kamau aliongeza kuwa Rais Mstaafu Kenyatta amewaambia wafuasi wake kuwa hatashiriki moja kwa moja kwenye siasa za 2027, na kwamba kila mmoja ana uhuru wa kujiunga na mrengo wowote.

Hii inathibitishwa pia na Mbunge Mteule, Bi Sabina Chege, ambaye alisema kuwa Jubilee imeachwa bila uongozi na wanajitahidi kujiimarisha upya.

Kundi la Jeremiah Kioni linaegemea upande wa Fred Matiang’i. Naye Mwenyekiti wa Jubilee, Torome Saitoti, yupo upande wa Gachagua.

Wengine kama Amos Mwago, Peter Mwathi, Jude Njomo, na Kabinga wa Thayu wamehamia DCP. Wafuasi wa Ruto kama Sabina Chege, Irene Njoki, na Kwenya Thuku wanasalia UDA.

Kwa kuwa Mlima Kenya una zaidi ya kura milioni 8, ni eneo muhimu sana katika kuamua mshindi wa urais.

Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa Kikuyu, Bw Wachira Kiago, alisema kuwa:

“Eneo la Mlima Kenya lina viongozi wawili: Mshauri Mkuu akiwa ni Kenyatta na Kiongozi wa Kisiasa akiwa ni Rigathi Gachagua.”

Aliongeza kuwa jamii iko tayari kusikiliza kila kiongozi kutoka kote nchini, lakini uamuzi wa mwisho utatolewa na wananchi