Akili MaliMakala

Watengenezaji wa chakula cha mifugo wahamasisha kilimo cha mahindi ya manjano kuziba pengo la malighafi

Na SAMMY WAWERU August 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MABADILIKO ya tabianchi, ukame wa muda mrefu na mvua zisizotabirika vinaendelea kuathiri uzalishaji wa mazao nchini Kenya, hali inayowasukuma watengenezaji wa chakula cha mifugo kuhimiza kilimo cha mahindi ya manjano ili kupunguza utegemezi wa malighafi kutoka nje na gharama za uzalishaji.

Chama cha Watengenezaji wa Chakula cha Mifugo Kenya (AKEFEMA) kinaitaka serikali, watafiti na wakulima kuhamasisha uzalishaji wa mahindi ya manjano kwa ajili ya chakula cha mifugo, huku mahindi meupe yakitengwa zaidi kwa matumizi ya binadamu.

“Malighafi huchangia kati ya asilimia 70 na 80 ya gharama ya kutengeneza chakula cha mifugo. Kenya bado inaagiza malighafi nyingi kutoka nje, licha ya kuwa na uwezo wa kuzalisha sehemu kubwa humu nchini,” alisema Mwenyekiti wa AKEFEMA Joseph Karuri.

Mahindi shambani yakiendelea kukua. Picha|Sammy Waweru

Karuri alisema mahindi ndiyo chanzo kikuu cha virutubisho vya wanga (carbohydrates) katika chakula cha mifugo, lakini uhaba wa mahindi kwa matumizi ya binadamu unalazimisha wafugaji kushindana na watu kwa nafaka hiyo.

Chama hicho pia kinataka kuongezwa kwa uzalishaji wa alizeti, soya, pamba na canola, ambazo mabaki yake baada ya kukamua mafuta hutumika kama chanzo muhimu cha protini katika chakula cha mifugo.

Karibu asilimia 80 ya malighafi hizo za protini huagizwa kutoka Tanzania, Uganda, Malawi na Zambia.

Kenya hutumia takriban magunia milioni saba ya mahindi ya kilo 90 kila mwaka kutengeneza chakula cha mifugo, sawa na tani 630,000. Ingawa uwezo wa viwanda vya kutengeneza chakula cha mifugo ni karibu tani milioni nne kwa mwaka, uzalishaji halisi ni tani milioni 2.5 pekee kutokana na uhaba wa malighafi.

Mkulima akikagua shamba lake la mahindi katika kaunti ya Kiambu. Picha|Sammy Waweru

Karuri alisema kuboresha lishe ya mifugo ni muhimu kuongeza uzalishaji wa maziwa, nyama na mayai. Kenya huzalisha karibu lita bilioni tano za maziwa kwa mwaka, lakini ng’ombe mmoja hutoa wastani wa lita saba hadi nane kwa siku.

Aidha, AKEFEMA pia inahimiza matumizi ya teknolojia ya Near Infrared (NIR), inayowezesha kuchanganua ubora wa malighafi ndani ya dakika tano hadi 10 na kusaidia wataalamu kutengeneza mchanganyiko sahihi wa chakula.

Makamu Mwenyekiti wa AKEFEMA, Dkt David Murumba, alisema teknolojia hiyo inaweza kupunguza upotevu wa malighafi wakati wa uundaji wa malisho, kuongeza ufanisi na kuboresha afya ya mifugo.

Chama cha Watengenezaji wa Chakula cha Mifugo Kenya (AKEFEMA) kinaitaka serikali, watafiti na wakulima kuhamasisha uzalishaji wa mahindi ya manjano kwa ajili ya chakula cha mifugo. Picha|Sammy Waweru

Katibu Mkuu wa AKEFEMA, Dkt Wilfred Kamau, alisema uwekezaji katika mashine za kisasa, wataalamu na mikopo nafuu ni muhimu kupunguza gharama za uzalishaji na hatimaye bei ya maziwa, mayai na nyama ya nguruwe kwa walaji pia itashuka.