Habari

Maswali, Ruto akimpiga kalamu mumewe Gavana Wanga

Na CHARLES WASONGA June 18th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto amemvua mumewe Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga, George Wanga, wadhifa wa Mwenyekiti wa Mamlaka ya Kusimamia Sekta ya Kawi na Petroli (EPRA) miezi mitano baada ya kumtunuka wadhifa huo muhimu serikalini.

Kupitia tangazo kwenye gazeti rasmi la serikali, toleo nambari 7850 la Juni 16, 2025, Dkt Ruto amemteua Bw Adan Haji Ali kujaza nafasi hiyo.

“Kwa mujibu wa mamlaka yaliyoko katika sehemu 12 (1) ya Sheria ya Kawi ya 2019, miye Rais William Samoei Ruto, Rais wa Jamhuri ya Kenya na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi yote, nimemteua Adan Haji Ali kuwa mwenyekiti wa  Mwenyekiti wa Mamlaka ya Kusimamia Sekta ya Kawi na Petroli kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia Juni 16, 2025. Uteuzi wa George Wanga umefutiliwa mbali,” akasema.

Bw Wanga, ambaye huwa ni nadra kuonekana hadharani, aliteuliwa katika wadhifa huo na Rais Ruto mnamo Januari 17, 2025 baada ya Rais Ruto kuanza kushirikisha serikalini wandani wa kiongozi wa ODM Raila Odinga alipobuni Serikali Jumuishi.

Alijaza nafasi iliyoachwa wazi kufuatia kufutwa kwa aliyekuwa Jaji wa Mahakama ya Juu Jackton Boma Ojwang’.

Gavana Wanga ni mwandani wa karibu wa Bw Odinga na ndiye mwenyekiti wa kitaifa wa chama hicho cha Chungwa.

Kando na hayo, huyo ameondokea kuwa mtetezi sugu wa ushirikiano wa kisiasa kati ya Rais Ruto na Bw Odinga, kiasi kwamba kiongozi wa taifa amezuru Homa Bay mara nane tangu alipoingia mamlaka 2022.

Kufutwa kwa Bw Wanga huenda kukaibua minong’ono kwamba huenda tofauti zimeanza kushuhudiwa katika serikali jumuishi haswa kufuatia kukithiri kwa visa vya ukatili wa polisi na mauaji ya kiholela.

Kwa mfano, viongozi wa ODM wamekuwa wakiishutumu serikali kuwa kuvumilia vitendo vya ukiukaji wa haki kufuatia kuuawa kwa mwanablogu Albert Ojwang’ katika seli ya kituo cha polisi cha Central, Nairobi.

Kifo hicho kimeibua kero kubwa nchini huku Wakenya wakifanya maandamano kushinikiza kukamatwa kwa Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi, aliyejiondoa kazini kwa muda, Eliud Lagat, aliyechangia kukamatwa kwa Ojwang nyumbani kwao Homa Bay Juni 7, 2025.