Habari za Kitaifa

Yaani hamjifunzi kitu? Shutuma zaendelea kurushwa kwa polisi

Na WAANDISHI WETU June 19th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

WAKENYA jana waliendelea kuchemnka kwa hasira kutokana na jinsi polisi walivyowakabili waandamanaji Jumanne ambapo mchuuzi wa barakoa alipigwa risasi kichwani na kunusurika mauti jijini Nairobi.

Mchuuzi huyo Boniface Kariuki alipigwa risasi kichwani na afisa wa usalama wakati wa maandamano ya kusaka haki kutokana na mauaji ya bloga na mwalimu Albert Ojwang’.

Japo ripoti ya awali ziliarifu alikuwa ameaga dunia, Bw Kariuki, 22 anapambania uhai wake katika Hospitali ya Kenyatta ambako amelazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi.

Risasi ya afisa huyo wa usalama ilimpata Bw Kariuki kichwani na kupita karibu na sikio lake akiwa karibu na Jumba la Imenti.

“Sote tunatoka Murangá lakini tunajitafutia riziki kupitia uchuuzi,” alisema babake John Kariuki Nyambura ambaye pia ni mchuuzi karibu na mzunguko wa Railways.

Bw John alisema huwa hawazungumzi mara kwa mara na mwanawe na alifahamu kuhusu masaibu yake mitandaoni kisha akayathibitisha na marafiki zake.

Msemaji wa Polisi Muchiri Nyaga jana alitoa taarifa kuwa polisi wawili wa cheo cha konstebo Barasa Masinde na Duncan Kiprono wametimuliwa kazini na kukamatwa kutokana na kisa cha kupigwa risasi kwa Bw Kariuki.

Wawili hao walikuwa wakizuiliwa kituo cha polisi cha Capitol Hill huku uchunguzi ukiendelea kabla ya kufikishwa mahakamani.

Jana, polisi walielekezewa lawama na kukashifiwa kutokana na kupigwa risasi kwa Bw Kariuki ambaye hakuwa amejihami.

Pia, matumizi ya magenge kuwakabili waandamanaji yalikashifiwa na kutajwa kama yanayokandamiza uhuru wa kuandamana.

Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili Nchini (LSK) Faith Odhiambo alishutumu kupigwa risasi kwa Bw Kariuki na kutaka hatua kali ichukuliwe dhidi ya magenge yaliyokuwa yamejihami kwa rungu yakipambana na waandamanaji.

“Tunakashifu ushirikiano wa polisi na wahalifu hao waliojirejelea kama kundi linalolinda jiji. Tunalaani tukio hili la polisi kushirikiana na magenge hayo kutatiza haki ya raia ya kuandamana,” akasema Bi Odhiambo.

Alifichua kuwa mmoja wa mawakili Ken Ochieng’ naye alivamiwa alipokuwa akienda kukutana na mteja wake.

“Amethibitisha kuwa wahuni waliompiga walishuka kutoka gari aina ya Land Cruiser la polisi kwenye barabara ya Koinange na walikuwa wakisindikizwa na wahudumu wa bodaboda,” akaongeza.

LSK ilitangaza kuwa imepata ripoti watu 17 walijeruhiwa wakati wa maandamano ya Jumanne.

Bi Odhiambo alishangaa kwa nini polisi ambao wanastahili kuwalinda waandamanaji sasa wamegeuka na kuwapiga risasi na hata kusaidiana na magenge kuwakabili wanaosaka haki.

Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Nchini Philip Anyolo naye alisema maovu ambayo polisi waliwatendea raia wakati wa maandamano ni ya kusikitisha na hayafai kutokea tena.

“Kumpiga risasi Mkenya ambaye hajajihami ni ukatili na unyama usiokuwa na kipimo,” akasema Askofu Anyolo ambaye pia anasimamia Dayosisi ya Nairobi.

“Magenge yaliyobeba rungu kushirikiana na polisi kuwapiga waandamanaji kisha kupora mali na kuharibu biashara za watu, ni jambo ambalo halifai kutokea. Tunawaomba vijana watulie na wasilipize kisasi dhidi ya maovu haya wanayotendewa na polisi,” akaongeza.

Kiongozi huyo wa kidini aliyaagiza makanisa yote ya Katoliki kote nchini yaombee waliojeruhiwa na nyoyo za walioangamia wakati wa maandamano nchini.

“Kutakuwa na ibada ambapo kando na kuombea waliojeruhiwa na walioaga, pia tutamwomba Mungu ashushe neema na huruma zake kwa nchi yetu. Tuongozwe na roho wa Mungu, Yesu Kristo wakati tunateseka kwa kupigania mambo mazuri na kwa njia sawa,” akasema.

Alikuwa ameandamana na Askofu Simon Peter Kamomoe na Kasisi David Kamau Ngángá.

Mamlaka Huru ya Kutathmini Utendakazi wa Polisi (IPOA) jana ilitoa takwimu zilizoonyesha kulikuwa na majeraha 13 kutokana na maandamano Jumanne.

IPOA ilisema inachunguza mienendo ya polisi na hata kupendekeza wapewe mafunzo kuhusu njia ya kistaarabu ambayo wanaweza kuitumia wakati wa maandamano ndipo wasiwajeruhi tu watu bila sababu.

Kuhusu mauti ya Bw Ojwang,’ IPOA ilisema imemwaagiza Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat afike mbele yake kuandikisha taarifa leo.

Bw Lagat ambaye alijiuzulu Jumatatu, ndiye alikuwa mlalamishi mkuu dhidi ya Bw Ojwang’ aliyedai alichapisha habari za kumchafulia jina.

Nje ya nchi, Uingereza nayo ilieleza wasiwasi wake kuhusu polisi kutumia nguvu kupita kiasi dhidi ya waandamanaji na kutoa wito wa kuchunguzwa kwa dhuluma hizo ili maafisa wa usalama waliozitekeleza waadhibiwe.

“Tunashughulishwa mno na ukatili dhidi ya waandamanaji uliodhihirika Jumanne na uchunguzi huru uendeshwe kuhusu yaliyotokea kisha hatua ichukuliwe. Polisi lazima wawe na maadili na kuwe na imani kutoka kwa raia katika wajibu wao badala ya ukatili ulioshuhudiwa,” ikasema taarifa kutoka ubalozi wa Uingereza nchini.

Haya yakiendelea, Msemaji wa Serikali Isaac Mwaura naye alikanusha madai kuwa polisi walikuwa wakishirikiana na magenge, akisema ni madai yanayolenga kuipaka tope serikali.

“Serikali ina maafisa wa usalama wa kutosha kuhakikisha sheria inadumishwa. Waliokuwa wakiendeleza uhalifu walikamatwa wakati wa maandamano na watafikishwa kortini,” akasema Bw Mwaura.

Ripoti za Daniel Ogetta, Ndubi Moturi, Kevin Cheruiyot