Matumaini Taita Taveta shehena ya kwanza ya madini ikifika kiwanda kipya cha chuma, Devki Steel Mills
KAUNTI ya Taita Taveta imepiga hatua muhimu katika azma ya kujikuza kiviwanda, baada ya shehena ya kwanza ya madini ghafi ya chuma kusafirishwa kutoka ranchi ya Kishushe hadi kiwanda cha kusindika madini hayo cha Devki.
Kiwanda hicho chenye thamani ya Sh11 bilioni kilicho Manga, Voi, kinatarajiwa kuzinduliwa rasmi mwezi ujao.
Hafla hiyo iliyofanyika Jumamosi iliashiria kuanza kwa shughuli za usafirishaji wa madini hayo, hatua ambayo viongozi na wakazi wa eneo hilo wameeleza kama mabadiliko makubwa kwa sekta ya uchimbaji madini na viwanda ya kaunti.
Gavana wa Taita Taveta Andrew Mwadime aliongoza hafla hiyo na kusema hatua hiyo inaonyesha mwanzo wa kuongeza thamani ya madini na inatarajiwa kufungua fursa za kiuchumi ambazo hazijatumika kwa miongo kadhaa.
“Huu ni mwanzo wa enzi mpya katika safari ya sekta ya madini ya Taita Taveta. Uzinduzi rasmi wa kiwanda cha kusindika madini ya chuma cha Devki mwezi ujao na Rais William Ruto utaimarisha zaidi nafasi yetu kama kitovu kinachochipuka cha viwanda,” alisema.
Bw Mwadime alieleza kuwa shughuli za uchimbaji madini eneo la Kishushe zinatarajiwa kuingizia kaunti mapato ya takriban Sh540 milioni kila mwaka, hali ambayo itaipa serikali ya kaunti rasilimali za ziada za kuboresha utoaji huduma na kuendeleza miradi.
Alisema mkakati wa kaunti wa kuendesha hamasisho kuhusu usindikaji wa madini ndani ya nchi badala ya kuyauza yakiwa ghafi nje, utazalisha maelfu ya nafasi za kazi, kuchochea biashara na kuongeza mapato ya wenyeji.
“Msukumo wetu wa uongezeaji thamani bidhaa unalenga kuhakikisha wananchi wetu wananufaika kikamilifu kutokana na rasilimali zinazopatikana ndani ya kaunti. Kusindika madini ya chuma papa hapa kutazalisha ajira, kuvutia wawekezaji na kubadilisha maisha ya wananchi,” akaeleza.
Kwa miaka mingi, sekta ya madini Taita Taveta imekabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo migogoro kuhusu mipaka ya maeneo ya uchimbaji, kucheleweshwa kwa mikataba ya ukodishaji na wasiwasi kuhusu utekelezaji wa wajibu wa kijamii wa wawekezaji kwa jamii zilizo maeneo ya uchimbaji.
Gavana Mwadime alisema ushirikiano kati ya serikali ya kaunti, serikali ya kitaifa, ranchi ya Kishushe na kamati maalumu umewezesha changamoto hizo kutatuliwa na kufungua fursa za utajiri mkubwa wa madini katika kaunti hiyo.
“Tunaweka Taita Taveta katika hadhi ya kuwa kitovu kikuu cha uchimbaji madini na viwanda Kenya kwa kuvutia uwekezaji, kuunda fursa na kubadilisha maisha ya wananchi wetu,” aliongeza.
Uzinduzi huo ulihusisha viongozi mbalimbali, wanachama wa Chama cha Ushirika cha Kishushe Ranch, wawekezaji na wadau katika kile ambacho wengi walitaja kuwa hatua ya kihistoria.
Kiwanda cha Devki ni miongoni mwa uwekezaji mkubwa zaidi wa viwanda katika eneo la Pwani na kinatarajiwa kuchangia pakubwa kuimarisha sekta ya utengenezaji wa chuma nchini.
Kitakapoanza kazi rasmi kitasindika madini ya chuma yanayochimbwa Kishushe, hatua ambayo itapunguza utegemezi wa mali ghafi kutoka nje ya nchi, na kupiga jeki ajenda ya serikali ya kukuza viwanda vya uzalishaji nchini.