Habari za Kaunti

Wawakilishi wa wadi waanza mchakato wa kutimua ofisini waziri wa kaunti

Na GEORGE MUNENE June 19th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

MADIWANI Kaunti ya Embu wameanza rasmi mchakato wa kumuondoa afisini Waziri wa Fedha wa Kaunti hiyo, Profesa Joe Kamaria, kwa madai kwamba anaidharau bunge la kaunti.

Madiwani hao wanamshutumu Prof Kamaria kwa kushindwa mara kwa mara kuwasilisha ripoti za utekelezaji wa bajeti kwa Bunge la Kaunti ya Embu na kukaidi wito wa kufika mbele ya Kamati ya Fedha ya Bunge hilo kujibu maswali kuhusu ukusanyaji wa mapato.

Ingawa Prof Kamaria alihudhuria kikao cha Kamati ya Bunge lote kilichoongozwa na Naibu Spika Ibrahim Swaleh (Kirimari), madiwani wanapendekeza achukuliwe hatua kwa mujibu wa Kifungu cha 22(3) cha Sheria ya Madaraka na Heshima za Mabunge ya Kaunti (2017), pamoja na Kifungu cha 40 cha Sheria ya Serikali za Kaunti kinachohusu kuondolewa kazini kwa maafisa wa kaunti.

Prof Kamaria alijipata katika hali ngumu kueleza ni kwa nini amekuwa akikwepa kufika mbele ya kamati za bunge la kaunti na kushindwa kuwasilisha ripoti za kila robo mwaka kuhusu matumizi ya fedha za umma zilizotengwa na bunge.

Madiwani walikasirika baada ya Prof Kamaria kuwatuma maafisa wa ngazi ya chini, wasiokuwa maafisa wa fedha wala watunga sera, kufika mbele ya kamati ya bunge kujibu maswali muhimu.

Walimlaumu profesa huyo kwa kudharau mamlaka ya bunge na kutowaheshimu wawakilishi wa wananchi, hali iliyowafanya wapendekeze kuondolewa kwake ofisini.