Likizo fupi yaanza walimu wakuu wakitua Mombasa
MAMILIONI ya wanafunzi wa shule za msingi na upili wataelekea nyumbani wiki hii kwa likizo fupi huku walimu wakuu wakikita kambi Mombasa kwa warsha yao ya kila mwaka kujadili masuala tata kuhusu elimu.
Wanafunzi hao watakuwa likizoni kuanzia Juni 25, 2025 hadi Juni 29, 2025 na kurejea shuleni kwa wiki nyingine tatu kumaliza silabasi na kujitayarisha kwa mitihani ya kufunga muhula wa pili.
Walimu hao wakuu wakiongozwa na Mwenyekiti wa Muungano wao wa kitaifa Willie Kuria alisema warsha hiyo itajumuisha zaidi ya walimu 9,000 ambao watakongamana katika ukumbi wa Sheikh Zayed Mombasa.
Mwaka huu, walimu hao watajadili namna ya kukumbatia mifumo ya elimu na matayarisho ya shule zao kupokea wanafunzi wa Gredi ya 10.
Wanafunzi milioni 1.2 walioko Gredi 9 wanaendelea na uchaguzi wa masomo yao na shule mbalimbali wanazotaka kujiunga nazo hapo mwakani baada ya kupewa mtihani wa kutathmini elimu yao ya shule ya msingi (KJSEA).
Walimu wa shule za kitaifa pia wanatakiwa kujitayarisha kuhusu namna wanafunzi wa kutwa watajiunga na shule zao.
Hii ni baada ya Wizara ya Elimu kutangaza kuwa shule za kitaifa zitatakiwa kuwa na wanafunzi wa kutwa ili kuhakikisha wanafunzi wote milioni 1.2 wanajiunga na shule za upili.
Awali, walimu wakuu walipinga mfumo huu wakisema itakuwa hatari hasa kwa masuala ya kudumisha nidhamu na hata wanafunzi wa kutwa kutumiwa kuingiza dawa za kulevya shuleni.
Masuala mengine ambayo yatajadiliwa ni pamoja na ufadhili wa masomo ya bure nchini.
“Waziri wa Fedha John Mbadi ataeleza kuhusu ufadhili wa masomo nchini. Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Kiteknolojia cha Mombasa, Prof Laila Abubakar, atajadili kuhusu namna ya kukumbatia teknolojia katika shule za upili,” alisema Bw Kuria.
Mkaguzi wa Hesabu za Serikali, Dkt Nancy Gathungu, naye atazungumzia namna ya kulinda fedha za elimu huku Tume ya Kuwaajiri wa Walimu Nchini (TSC) ikitwikwa jukumu la kueleza kuhusu nafasi ya walimu katika kusaidia wanafunzi kuchagua masomo ya shule za sekondari.
Waziri wa Afya, Bw Aden Duale, ataeleza kuhusu afya ya wanafunzi shuleni.
Mnamo Juni 25, Naibu Rais Prof Kithure Kindiki atafungua rasmi kongamano hilo ambalo litahudhuriwa pia na wageni tofauti akiwemo Mwenyekiti wa TSC Dkt Jamleck Muturi, Gavana wa Mombasa Bw Abdulswamad Nassir, Waziri wa Elimu Bw Julius Ogamba.
Ufadhili wa masomo umesalia donda sugu nchini huku walimu wakuu wakilalamika kwa kusema serikali imepunguza bajeti.
Hata hivyo, kamati ya bunge inayosimamia elimu ikiongozwa na mwenyekiti wake Bw Julius Melly alisema bajeti hiyo inatosha kuhakikisha elimu inapigwa jeki.