Michezo

SportPesa yafadhili 2026 Sevens Circuit kwa Sh34 milioni

Na CECIL ODONGO June 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MZUNGUKO wa Kitaifa wa Raga ya Wachezaji Saba (National Sevens Circuit) 2026 ulipigwa jeki wiki hii baada ya SportPesa kutangaza ufadhili wa Sh34.14 milioni.

Tangazo la ufadhili huo lilikuja wiki chache kabla ya kuanza kwa makala ya 25 ya mzunguko utakaoanza Julai 25 na 26 kwa mashindano ya Prinsloo 7s jijini Nakuru.

Msururu huo wa raundi sita kisha utaelekea Kisumu, Nairobi, Mombasa na Embu kabla ya kuhitimishwa na Christie 7s jijini Nairobi Septemba.  Akizungumza wakati wa uzinduzi wa ufadhili huo, Mkuu wa kitengo cha mauzo SportPesa, Willis Ojwang, alisema ushirikiano huo ni zaidi ya ufadhili wa kifedha, akisifia ushirikiano wa miaka minne kati ya SportPesa na raga ya Kenya.

“Hili si suala la udhamini pekee bali pia linahusu ushirikiano na kukuzwa kwa mchezo wa raga,” akasema Ojwang.  Kati ya fedha hizo, Sh6 milioni zitatolewa kusaidia klabu zitakazoandaa mashindano, huku Sh6 milioni nyingine zikielekezwa kwa Muungano wa Raga Kenya (KRU).

Aidha, Sh9 milioni zitatumika katika matangazo ya vyombo vya habari, masoko na uperushaji wa moja kwa moja wa mashindano.  Pia, Sh4.14 milioni zimetengwa kwa zawadi za washindi, ongezeko kubwa kutoka Sh1 milioni zilizotolewa mwaka jana.

Katika kila raundi ya Daraja la Kwanza, timu za wanaume zitakazoshika nafasi ya kwanza zitapata Sh150,000, nafasi ya pili Sh75,000 na nafasi ya tatu Sh40,000.  Kwa upande wa wanawake, washindi watapata Sh100,000, washindi wa pili Sh50,000 na wanaomaliza wa tatu Sh25,000.

Washindi wa Daraja la Pili pia watanufaika, ambapo timu itakayoshika nafasi ya kwanza itapata Sh70,000 huku ya pili ikijinyakulia Sh30,000.

Mabingwa wa jumla wa mzunguko huo pia watapata zawadi zilizoongezwa. Kwa wanaume, washindi watapata Sh300,000, nafasi ya pili Sh150,000 na nafasi ya tatu Sh100,000.

Kwa wanawake, mabingwa watazawadiwa Sh200,000, washindi wa pili Sh100,000 na nafasi ya tatu Sh50,000.   Mbali na zawadi za mashindano, SportPesa imetenga Sh2 milioni kwa ajili ya ununuzi wa bidhaa rasmi za mzunguko huo.

Baada ya raundi ya ufunguzi mjini Nakuru, timu zitaenda Kisumu kwa mashindano ya Dala 7s yatakayofanyika Agosti 1 na 2.  Kisha mzunguko utarejea Nairobi kwa Kabeberi 7s mnamo Agosti 15 na 16 kabla ya kuelekea Mombasa kwa Driftwood 7s Agosti 22 na 23.

Raundi ya mwisho kabla ya fainali itafanyika Embu Septemba 5 na 6, kabla ya msimu kutamatika Christie 7s jijini Nairobi mnamo Septemba 12 na 13.