Familia ya Boniface Kariuki yataka kuambiwa ukweli kuhusu hali yake
FAMILIA ya Boniface Kariuki, mchuuzi wa barakoa kutoka Murang’a ambaye alipigwa risasi kichwani na afisa wa polisi wakati wa maandamano wiki moja iliyopita, inasubiri majibu kuhusu hali yake kutoka madaktari.
Boniface, mwenye umri wa miaka 22, ameweka familia yake katika msongo wa mawazo kwa zaidi ya wiki moja, akilazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU) katika hospitali ya Kenyatta, akiwa kwenye mashine ya kumsaidia kuwa hai.
Mama yake Susan Njeri, anasema hawajapata maelezo kamili kutoka kwa madaktari kuhusu hali ya mwanawe, jambo linalozua wasiwasi mkubwa kwa familia.
“Wakati mtu yuko kwenye mashine ya kumsaidia kupumua, huwezi kusema kama yuko hai au amekufa. Tunataka daktari atueleze ukweli. Kuna mambo mengi yanayosemwa mitandaoni lakini hatuna chochote kutoka kwa madaktari. Hatujui tuamini nini,” alisema mama yake, Susan Njeri, katika mahojiano nyumbani kwao Nduni, Kaunti ya Murang’a.
Wanashirikiana na Mamlaka ya Usimamizi wa Polisi (Ipoa) kuhakikisha haki inapatikana.
Familia inaomba uchunguzi wa kina na uwazi kuhusu tukio hilo ili kumaliza hofu na maswali yanayowazunguka.
Licha ya mazungumzo mengi na maafisa wa serikali, ikiwa ni pamoja na maafisa wakuu wa polisi waliowatembelea familia Jumatatu, Bi Njeri amesema hawajapokea msaada wala majibu ya wazi.
“Tunahisi kama tunajizungumzia wenyewe tu. Mikutano isiyoisha, mahojiano ya vyombo vya habari bila mwisho lakini hakuna anayetuambia hali ya Boniface ni gani,” alisema Bi Njeri, akiongeza kuwa hadi Juni 21, bili ya hospitali ilikuwa imefikia Sh1.5 milioni.