Habari za Kitaifa

Kindiki, Murkomen wakemea makanisa, mabalozi kwa ‘kuchochea maandamano ya ghasia’

Na MERCY SIMIYU, PIUS MAUNDU June 27th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WAZIRI wa Usalama wa Ndani, Kipchumba Murkomen na Naibu Rais Kithure Kindiki wamekemea vikali jamii ya kimataifa na makanisa nchini kwa kile walichosema ni upendeleo na kuingilia masuala ya kisiasa ya Kenya bila kufanya uchunguzi wa kina.

Akizungumza kwa hasira kwenye mkutano na wanahabari nje ya Jumba la Harambee, jijini Nairobi, Alhamisi, Murkomen alishutumu mataifa ya kigeni kwa kujaribu kuingilia uhuru wa Kenya, akidai hawataki kuona nchi ikiwa salama na demokrasia kamili.

Waziri Murkomen alilaumu viongozi wa makanisa “wanaochochea ghasia badala ya kuwasilisha sauti ya busara inayohitajika katika kushughulikia changamoto za kijamii.”

“Ninajua hakuna askofu wala kiongozi wa kanisa yeyote, iwe wa Kanisa Katoliki au Anglikana, atakayesimama kutetea polisi. Hakuna atakayezungumzia majeraha ya polisi. Na pia ninajua hakuna mwanadiplomasia atakayekemea hayo. Hii ni kwa sababu hawataki kuona Kenya ikiwa salama,” Murkomen alisema kwa ukali.

Waziri huyo, ambaye ni wakili kitaaluma, alisema polisi walivumilia sana licha ya kuchokozwa na vijana waliokuwa wakishiriki maandamano. Aliwahakikishia maafisa wa polisi kuwa serikali itawatetea dhidi ya mashambulizi kutoka kwa wanahabari, kanisa, na mataifa ya nje.

“Ninawapongeza polisi wetu kwa kufanya kazi nzuri ya kuokoa nchi na ninataka kuwahakikishia kwamba ninawaunga mkono kwa dhati,” alisema Bw Murkomen.

Katika taarifa yake, Waziri huyo  pia alifichua kuwa serikali imeanza uchunguzi ili kubaini wahusika waliowafadhili waandamanaji, akisema baadhi ya matukio ya siku ya maandamano yaliashiria jaribio la mapinduzi ya serikali na ugaidi.

“Nilikuwa katika kituo cha ufuatiliaji maandamano yalipokuwa yakiendelea. Tayari nimemwelekeza Mkuu wa Polisi, Douglas Kanja, aanzishe uchunguzi kuhusu visa vya uporaji ambavyo vilitokea katika maeneo mengi ya jiji la Nairobi,” alisema Murkomen.

Kwa mujibu wa waziri huyo, maafisa wa polisi 300 walijeruhiwa huku raia 100 pia wakipata majeraha. Vituo kadhaa vya polisi viliteketezwa huku bunduki tano zikiibwa kutoka kituo cha Dagoretti, Kaunti ya Kiambu, na zingine nne ziliteketezwa katika kituo kingine cha polisi.

Bw Murkomen aliongeza kuwa maandamano ya Juni 25 yaliacha watu zaidi ya 10 wakiwa wamefariki, huku baadhi ya wahalifu wakijiunga na maandamano wakilenga kuvamia miundomsingi ya usalama kama vituo vya polisi.

Zaidi ya magari 27 ya serikali ya kitaifa na kaunti pamoja na magari ya kiraia 65 yaliyokuwa yameegeshwa katika vituo vya polisi yaliharibiwa.

“Mabohari ya biashara, maduka ya vifaa vya elektroniki, hoteli, mikahawa na hata nyumba za watu binafsi zilivamiwa na kuchomwa. Mojawapo ni mali ya Kanisa Katoliki huko Kaunti ya Embu,” Murkomen alidai.

Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki aliwalaumu viongozi wa makanisa, mabalozi na wanasiasa wa upinzani kwa kuchochea maandamano ya vijana dhidi ya serikali.

Akizungumza kwa ukali mjini Kambu, Kaunti ya Makueni, Prof Kindiki alisema serikali haitakubali maandamano ya namna hiyo kurudiwa tena, akiyataja kuwa ya kihuni na yenye madhara makubwa kwa taifa.

“Nikiwa mtu ambaye nimekuwa kwenye siasa kwa muda mrefu, naweza kusema kwa hakika kuwa siku ya jana ilikuwa ya vurugu zaidi katika historia ya nchi yetu tangu machafuko ya baada ya uchaguzi wa 2007/08. Ilikuwa ni aibu kubwa. Kupoteza maisha, uharibifu wa mali ya umma na binafsi, uporaji wa waziwazi, na kuharibiwa kwa biashara ni mambo ambayo hayajawahi kushuhudiwa,” alisema Prof Kindiki.

Naibu Rais alikuwa katika eneo hilo kuongoza harambee ya kuwasaidia vikundi vya wanawake na vijana, huku akiandamana na wandani wa Rais William Ruto.

 “Tunaendelea kutathmini hali baada ya ghasia. Vituo vya polisi viliteketezwa, bunduki na risasi zikaibwa. Hii ni thibitisho kuwa kulikuwa na nia fiche zaidi ya malalamishi yaliyotajwa hadharani. Ndiyo maana nasema, kamwe hatutaruhusu nchi yetu itumbukie katika machafuko,” aliongeza Prof Kindiki.