Habari

Walimu wakuu kuhojiwa bungeni kuhusu fedha shuleni

Na WINNIE ATIENO July 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WALIMU wakuu wa shule za upili za umma nchini wataanza kufikishwa mbele ya Bunge la Kitaifa kueleza jinsi walivyotumia mabilioni ya fedha za umma, katika hatua mpya ya kuimarisha uwajibikaji katika sekta ya elimu.

Kamati ya Elimu Bungeni imesema itaanza kwa kuhoji wakuu wa shule za Kundi C1 (zamani shule za kitaifa), kabla ya kufanya zoezi hilo kwa shule za C2 (Extra County), C3 (County) na C4 (Day Schools) kote nchini.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Dick Maungu, alisema uamuzi huo umechochewa na ripoti za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali zinazoonyesha kuwa shule nyingi zinazopokea fedha nyingi za umma hazijawahi kufika bungeni kujibu maswali kuhusu matumizi yake.

Alisema Bunge limeandaa mfumo utakaowawezesha wakuu wa shule kujibu moja kwa moja hoja zilizoibuliwa katika ripoti za ukaguzi.

Shule za Kundi C1 hupokea fedha za serikali kupitia mgao, hukusanya karo kutoka kwa maelfu ya wanafunzi na pia husimamia miradi ya maendeleo yenye thamani ya mamilioni ya pesa.

Bw Maungu alisema kuna pengo kubwa la usimamizi kwa kuwa taasisi ndogo kama Vyuo vya Kiufundi (TVET) huhojiwa na Bunge mara kwa mara, ilhali shule kubwa zenye wanafunzi zaidi ya 2,000 na bajeti kubwa hazijawahi kufanya hivyo.

Hatua hiyo inajiri wakati shule nyingi zinakabiliwa na uhaba wa fedha kutokana na kuchelewa kwa mgao wa serikali.

Hali hiyo imezifanya shule kushindwa kulipa madeni, kuchelewesha malipo kwa wawasilishaji bidhaa na wakati mwingine kuwarudisha wanafunzi nyumbani kwa sababu ya karo.

Waziri wa Elimu Julius Ogamba aliunga mkono hatua hiyo akisema itaimarisha uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma.

Mwenyekiti wa Chama cha Kitaifa cha Wazazi, Silas Obuhatsa, alisema hatua hiyo itasaidia kurejesha imani ya wananchi lakini akaonya isiwe njia ya kuwanyanyasa wakuu wa shule.

Kwa upande wao, wakuu wa shule kupitia mwenyekiti wa KESSHA, Willie Kuria, walisema wako tayari kujieleza mbele ya Bunge.