LAWAMA ZAANZA: Wabunge wa Ruto wataka Gachagua akamatwe kuhusu ghasia za GenZ
KUNDI la wabunge wa Kenya Kwanza na ODM sasa linataka aliyekuwa naibu rais, Rigathi Gachagua akamatwe wakidai ndiye kiini cha machafuko yaliyogubika maandamano ya GenZ, Jumatano.
Wakihutubia vyombo vya habari Alhamisi katika majengo ya Bunge, wabunge hao wanaogemea serikali pana walimshutumu naibu rais aliyefurushwa kwa kufadhili ghasia zilizosababisha vifo, majeraha na uharibifu wa mali katika kaunti kadhaa kote nchini.
Wabunge hao wanaojumuisha Didimus Barasa (Kimilili), Mark Nyamita (uriri), Japheth Nyakundi (Kitutu Chache) Ali Wario (Bura) na waakilishi wanawake Lilian Sioi (Trans Nzoia), na Fatuma Mohammed (Migori) walimshutumu Bw Gachagua kwa kutumia magenge ya wahuni kushinikiza siasa za kikabila Mlima Kenya.
“Tunaitisha aliyekuwa naibu rais aliyefurushwa kukamatwa. Amerekodiwa akichochea vita na vijana wetu dhidi ya wanaokataa kufuata mtazamo wake wa siasa duni,” alisema Mbunge wa Kimilili.
Bw Barasa alihoji kuwa, hali kwamba sehemu kubwa ya uharibifu wa mali iliathiri Eneo la Kati, linalochukuliwa kuwa ngome ya Bw Gachagua ni ishara tosha kuwa,” naibu rais wetu aliyefurushwa amekuwa akikusanya raslimali na wahuni kuvamia mali ya serikali na hasa kuwalenga watu binafsi na biashara zinazomilikiwa na wasiofuata msimamo wake kisiasa.”
Kauli yake ilirejelewa na Mwakilishi Mwanamke Trans Nzoia aliyesisitiza maandamano ya vijana yaliyodhamiriwa kuwakumbuka vijana wanarika GenZ waliouawa Juni 25, mwaka jana, yalikuwa jaribio la kupindua serikali.
“Hayo hayakuwa maandamano, yalikuwa mapinduzi. Aliyepanga alikusudia kupindua serikali ya William Ruto. Tunataka sheria ichukue sheria kikamilifu,” alisema Bi Mohammed.
Kulingana na mbunge huyo, “maafa yaliyofanyika jana ni ya kujitakia kwa sababu mliambiwa vizuri mfanye maandamano ya kikatiba lakini ilikuwa ujambazi, na ilikuwa watu wabinafsi” akiashiria lawama jamii moja.
Kuhusu ukatili wa polisi na utekaji nyara, wabunge haoi walisisitiza kuwa maafisa wa polisi ni sharti waruhusiwe kufanya kazi yao huku wakiwashutumu wanaharakati wa kutetea haki za kibinadamu kwa kupendelea wahalifu.
“Ni nani anayewalinda polisi? Tusiwe tunatetea uhalifu tu. Kama walikuwa wanaadhimisha, kumekuwa na vifo vingi kama 2007/2008 ambapo watu zaidi ya elfu moja waliangamia. Tukisema kila wakati maovu yanafanyika tuwe tukiandamana, ni lini tutafanya kazi kama nchi?”Alihoji Bi Sioi.
Wabunge sasa wanatishia kuwasilisha mswada bungeni na kufunga baadhi ya mashirika ya wanaharaki kwa wanachotaja “kuwatumia Wakenya vibaya.”
“Polisi mwanamke au mwanamme ni binadamu pia. Mbona hamjaandamana kuwatetea maafisa wa polisi waliojeruhiwa katika tukio hili ili kutetea haki zao vilevile. Je, haki ni za raia pekee” Wanaharakati tumewapa notisi, hamtawatumia Wakenya na kujiundia hela kutokana na matukio mabaya,” alisema Bi Mohammed.
“Huwezi kuwa unaona polisi anachapwa hapo unanyamazia halafu jambazi mmoja akipigwa risasi unakimbia kortini. Hawa wote waliokuwa hapo, viongozi sijui majaji, jaji mkuu wa zamani naye miaka 20 iliyopita nikiwa mtoto na hakufanya badiliko hata moja la kisheria lakini hii leo ako barabarani na vitukuu na wajukuu wake yeye ni GenZ,” alihoji mbunge huyo akisisitiza kuwa rais “Ruto haendi kokote, yuko hapa kudumu.”