Habari

Visa vya mauaji: Matiang’i atishia kumwaga mtama

Na MWANGI MUIRURI June 28th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiangí amesema kuwa sasa yuko tayari kumwaga mtama kuhusiana na mauaji ya kiholela na kutupwa kwa miili ya watu kwenye Mto Yala wakati wa utawala wa Rais Uhuru Kenyatta.

Dkt Matiangí amesema kuwa atachukua hatua hiyo ili isiwe ni ni yeye tu ambaye atakuwa anaangaziwa bali mchakato wote uanzie 1963 taifa lilipojinyakulia uhuru.
Katika serikali iliyopita, Dkt Matiangí alihudumu kama waziri wa usalama wa ndani mnamo Januari 2018 hadi Septemba 13, 2022 wakati ambapo Rais William Ruto alichukua mamlaka.
Tayari waziri huyo wa zamani ametangaza azma yake ya kuwania urais 2027 huku Bw Kenyatta akidaiwa kumuunga mkono hasa ikizingatiwa chama cha Jubilee kimetangaza atakuwa mwaniaji wao.
Alipokuwa akihudumu kwenye utawala uliopita, baadhi ya vifo tatanishi vilivyotokea vilikuwa ni vya afisa wa cheo cha sajini Kipyegon Kenei mnamo 2020, Meneja wa Teknolojia kwenye Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC) Chris Msando mnamo 2017 na mfanyabiashara wa dhahabu Jacob Juma mnamo 2016.
Hata hivyo, Dkt Matiangí anasema kuwa hawezi kusulubishwa pekee yake kutokana na matukio haya kwa sababu kuna waliohudumu hapo awali na lazima wawajibikie maafa ya nyuma.
“Njia pekee ni tuwe na ukweli kuhusu majukumu yetu na kufanya mambo sawa kwa nchi yetu. Hatufai kuegemea tu uchunguzi kuhusu matukio yaliyofanyika hivi majuzi pekee, turejee nyuma na tufahamu yaliyotokea tangu uhuru 1963,” akasema kupitia taarifa kwa umma mnamo Juni 26, 2025.
“Ni baada tu ya kila kitu kuchunguzwa na kusikizwa ndipo tunaweza kufahamu ukweli kuhusu Msando, Juma, Keni na Mto Yala. Uchunguzi ufanywe wa wazi kuhusu mauaji haya na yale yaliyotokea hapa awali ili tusonge mbele,” akaongeza Dkt Matiangí.
Mnamo Alhamisi, Dkt Matiangí akiwa ameandamana na Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka na mwenzake wa DAP K Eugene Wamalwa, walikashifu mauaji ya zaidi ya watu 15 wakati wa maandamano ya Juni 25.
Maandamano hayo yalikuwa ya kuadhimisha mwaka mmoja tangu mauaji ya zaidi ya vijana 60 mwaka jana, wakipinga Mswada wa Fedha 2024.
“Hii sasa imekuwa hadithi na tunaweza kuzuia maafa yaliyotokea yasitokee tena. Ni vyema tutumie muda wetu kuyashughulikia masuala mengine badala ya hili suala,” akaongeza.
“Wakati mwingine mambo hutokea kisha huyatumia kwa ajili ya kutimiza maslahi na ajenda za kisiasa. Sote tuliosimama hapa (Musyoka na Wamalwa) tumehudumu kama mawaziri na lazima tujitokeze kuzungumzia majukumu yetu ili masuala haya yasitumike kusaka umaarufu wa kisiasa,” akasema.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha JKUAT, Bw Charles Mwangi hata hivyo anasema kauli ya Dkt Matiangí inaonyesha kuwa hayuko tayari kuchunguzwa kuhusu mauaji yaliyotokea akiwa madarakani.